The House of Favourite Newspapers

Raha ya mapenzi, kudamka!

HAYA tena shoga yangu, kujifanya kuvamia sherehe za watu na dera la msiba kimbelembele hadi wka bi harusi inahu? Hivi jamani kwani lazima kila koki ni ya kufungua? Na utajiuliza sana hiyo kudamka veeepe! Shoga kama ulizoea kujiwekea kucha za bandia wakati unajua kuna kufua mbona utachuuuna! Vijana wa leo wanakwambia hata lori la mkaa nalo ni la kuogopwa! Heee heeeiyaaaa!

Leo nimekuja na kitu cha moto mashosti zangu chenye lengo la kuwaunguza wanaolea tabia ya uvivu wa kudamka kitandani, wakimuacha mume akiamka na kujiandalia kila kitu. Najua imeanza kukuingia akilini! Hivi nikuulize shoga, huoni aibu mume kukuacha kitandani kisha akajihudumia kila kitu mwenyewe wakati wewe ni mzima na huna tatizo lolote?

Wanawake wa siku hizi ndoa zinatushinda kwa sababu tunapenda kushindana na wanaume, eti akikwambia mke wangu kaniwekee maji ya kuoga, unamwambia umechoka, jana umelala saa sita, hivi unadhani ni sawa shosti? Nakukumbusha, kitanda ulikiacha kwenu na kama unaweza kuiheshimu ofisi ukaamka mapema kuikimbilia, hivi unashindwa nini kuamka mapema kwa ajili ya mumeo?

Ndoa inatafutwa bibi, nakusihi sana ulikumbuke hilo kabla ya kuja kujuta baadaye, maana ukishaachwa utaanza kumtafuta mchawi wakati umejiroga mwenyewe. Wanawake wenzangu niwakumbushe tu kitu kidogo, raha ya mapenzi ni kudamka asikwambie mtu shoga! Mume ni kama mtoto mchanga, anahitaji malezi hivyo ni jukumu lako kudamka asubuhi na mapema kabla yeye hajatoka kitandani ili umuandae vizuri hata kama haendi kazini.

Hivi mumeo kaamka, kaenda zake kaoga kaingia jikoni kajitengenezea chai, unapoamka unamkuta akinywa huku anatazama televisheni sebuleni, unajisikiaje? Halafu anakuuliza leo tutakula nini? Wakati muda huo wewe hata mswaki hujapiga mtoto wa kike, hivi na akili zako utalijibu swali hilo?

Niwakumbushe mashostito, msingi wa familia bora ni pamoja na mienendo ya nyumba yenu, kuanzia imani za kidini na malezi kwa ujumla, imani zote zinamkumbusha mwanadamu kuamka na kumuomba Mungu kabla hajafanya lolote. Kama wewe ni mama wa nyumbani, mumeo na watoto wakishaondoka, huo ni wakati wako wa kurudi kitandani kumalizia usingizi wako.

Tujiangalie, huenda ndani ya kichwa chako kuna shetani, mkemee aondoke, ijenge ndoa yako kwa sababu ikitokea siku mumeo akampata mtu wa kumpetipeti, umekwisha! Kwa leo acha niishie hapa tukutane tena siku nyingine. Ni mimi Shangingi Mstaafu ukipenda waweza niita Anti Nasra!

Comments are closed.