The House of Favourite Newspapers

Robertinho Atua Dar Alfajiri, Amficha Kipa Mpya! Msemaji wa Simba Atamba

0

KOCHA Mkuu wa Simba Mbrazili, Roberto Oliveira ‘Robertinho’ ametua nchini akitokea nyumbani kwao Brazil alipokwenda katika mapumziko.

Mbrazili huyo amerejea nchini mara baada ya kumalizika mapumziko ya siku kumi kwake na wachezaji wa timu hiyo, tayari kwa ajili ya maandalizi ya msimu ujao.

Kikosi hicho hivi sasa kipo katika maandalizi ya kambi inayotarajiwa kuwa nchini Uturuki na itakwenda huko kwa ajili ya kujiweka fiti kwa msimu ujao.

Championi Jumatano, linafahamu kuwa kocha huyo alitarajiwa kutua nchini akiongozana na kipa mpya wa timu hiyo, Mbrazili anayeitwa Caique Luiz Santos da Purificacao akitokea Klabu ya Ypiranga RS inayoshiriki Ligi Daraja la Pili nchini Brazil.

Caique Luiz Santos da Purificacao

Akizungumza na Championi Jumatano, Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa timu hiyo, Ahmed Ally alisema kuwa mara baada ya kocha kurejea jana alfajiri, nao wachezaji wao wa kigeni na wazawa walitarajiwa kuripoti kambini kuanzia jana Jumanne.

Ally alisema kuwa, tayari wachezaji wazawa wamesharipoti huku wakigeni wakitarajiwa kutua nchini kuanzia leo Jumatano tayari kwa ajili ya mandalizi ya safari ya kuelekea Uturuki ambako watapiga kambi ya msimu 2023-24.

Aliongeza kuwa timu itaondoka kati ya Jumanne au Jumatano ijayo mara baada ya taratibu zote kukamilika za safari ikiwemo utambulisho wa wachezaji wapya unaotarajia kuanza leo Jumatano.

“Tunakwenda Uturuki kuweka kambi fupi ya ya wiki tatu kwa ajili ya kujiandaa na msimu mpya wa 2023-24 ambao unakwenda kuwa bora kwetu Simba.

“Timu itaondoka na kikosi kamili kilichosajiliwa kwa msimu ujao chini ya Kocha Robertinho na benchi zima la ufundi litakalokuwepo.

“Na kuhusu huyo kipa Mbrazili, bado sijapata taarifa zake kuwa amekuja na kocha Robertinho au vipi, lakini tuwaambie kuwa kuanzia kesho (leo) Jumatano tutambulisha mchezaji mmoja mkubwa,” alisema Ally.

STORI NA WILBERT MOLANDI

Leave A Reply