The House of Favourite Newspapers

Simba washusha Majembe Mapya

MABOSI wa Simba kwa msimu ujao hawataki mchezo kwani wamedhamiria kukisuka hasa kikosi chao kiwe cha ushindani na kwa kuanza hivi karibuni watazishusha sura mpya nne za kigeni, akiwemo mshambuliaji Mzambia, Lazarus Kambole.

 

Mabosi wa Simba wanataka kukiboresha kikosi chao kwa kuleta wachezaji wenye viwango vikubwa kutokana na aina ya matokeo ambayo walikuwa wanayapata kwenye michezo ya Ligi ya Mabingwa Afrika ya ugenini kwa msimu huu.

 

Chanzo kutoka Simba kimeliambia Championi Jumatatu, kuwa wachezaji hao wane wanatarajiwa kuingia nchini hivi karibuni ambapo wanaweza kuwemo kwenye mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya Simba na Sevilla ya Hispania.

 

“Viongozi wanataka kuboresha kikosi kiwe na uwezo wa hali ya juu kwenye michezo ya kimataifa kuliko msimu huu, ndiyo maana viongozi wanaleta wachezaji wenye uwezo wa hali ya juu kuliko ambao wapo kwa sasa.

 

“Wachezaji hao wanaweza kuwepo hapa nchini kwenye mechi na Sevilla kwa ajili ya kuangaliwa na kuongea na viongozi kabla ya kusaini mikataba kwa msimu ujao.

 

“Huyo Kambole unayesema anaweza kuwemo katika orodha hiyo, lakini ni suala la kusubiri kuona kama ni yeye ambaye atakuja hapa ama la,” kilisema chanzo hicho.

 

Katibu wa Simba, Anord Kashembe amesema: “Huu siyo wakati wa kufanya usajili, hatuwezi kulizungumzia hilo, ukifika muda wake kila kitu kitakuwa sawa.”

Comments are closed.