The House of Favourite Newspapers

Timu ya Taifa ya Kikapu Yawaangukia Watanzania

Rais wa shirikisho la mpira wa kikapu nchini  (TBF) Fares Magesa na wachezaji wawili, Ally Mbegu na Fatma Yassoda, walipotembelea +255 Global Radio katika ofisi za Global Group zilizoko Sinza-Mori, jijini Dar es Salaam..

TIMU ya taifa ya mpira wa kikapu ya wanaume na wanawake imewaomba Watanzania kuwachangia fedha ili iweze kumudu gharama za kwenda Uganda kushiriki mashindano ya Kanda ya Tano (FIBA Zone V) yaliyopangwa kufanyika Juni 25 mwaka huu.

 

Hayo yalisemwa na Magesa akiambatana na wachezaji wawili, Ally Mbegu na Fatma Yassoda, ambapo leo walifanya ziara katika ofisi za Global Group zilizopo Sinza-Mori,  Dar,  na kufanya mahojiano na Global TV Online  na +255 Global Radio kupitia kipindi cha michezo cha Jumamosi (Kick Off) na kusifu mwonekano na ubora wa studio hizo ambapo alitoa wito huo kwa Watanzania  ili waweze kusafiri Juni 23 kwenda Uganda.

Magesa akizungumza jambo katika ofisi za Global Group.

Timu hio inatarajiwa kuondoka tarehe 23 na wachezaji 24, makocha wawili kila timu,  madaktari na viongozi wa TBF ambapo idadi yao inafikia 33 na wanahitaji kiasi cha Sh. milioni 57 ili kufanikisha safari hiyo ambapo kiasi hicho kitatumika kwenye kuwasafirisha, kuwapataia malazi, chakula na posho za wachezaji na viongozi.

 

“Tunaomba Watanzania  watusaidie michango yao ya hali na mali kwa sababu tunatakiwa kwenda Uganda kushiriki mashindano ya (FIBA Zone V) ambayo yatatusaidia kupata tiketi ya kwenda kushiriki mashindano ya FIBA Afrika.  Wachezaji wote wapo tayari kwa mashindano ila kikwazo ni kupata pesa kwa ajili ya safari hiyo, hivyo kwa yeyote ambaye atataka kutuma chochote anaweza kutuma  kupitia namba 0715 969567.

Magesa katika studio za +255Global Radio.

“Siyo lazima watu watoe pesa, tunapokea vifaa vya michezo, tiketi za safari, maji, chakula na hata kama kuna ambaye atajitolea kutupatia sehemu ya kulala kule Uganda itakuwa jambo nzuri sana, hivyo tunatoa rai kwa serikali, wabunge, viongozi wote na wananchi kwa ujumla wake kuweza kutuchangia ili tufanikishe safari hiyo, kwa sababu wachezaji wetu wakubwa kama Hasheem Thabiti amekubali kuja kushiriki mashindano hayo,” alisema Magesa.

 

Kwa upande wake, Yassoda aliyewakilisha timu ya wanawake alisema: “Kwa upande wetu sisi kama wachezaji tumejiandaa vizuri na tupo tayari kwa ajili ya mashindano ila tunachoomba Watanzania watusaidie kupata shilingi milioni 57 ili tuweze kufika Uganda.”

Magesa na  Yasoda wakiongea na Meneja Mkuu wa Global Publishers,  Abdallah Mrisho.

Mbali na kufanya mahojiano, Magesa na wachezaji wake walipata nafasi ya kukutana na Meneja Mkuu wa Global Publishers, Abdallah Mrisho,  ambaye aliahidi kutoa msaada kwa timu hizo kuanzia matangazo na kuhakikisha kiasi hicho cha pesa kinapatikana na timu inasafiri kwenda Uganda.

 

“Sisi kama Global Group tutatoa msaada wetu kuanzia sasa hadi pale ambapo suala hili litakapokamilika na tutahakikisha mnapata msaada wote ambao mtakuwa mnahitaji kutoka kwetu,” alisema Mrisho.

Comments are closed.