The House of Favourite Newspapers

Tujifunze wenzetu wanavyoendesha ligi zao

Msimu huu ambao unakamilika Mei 28 ni wakati sahihi wa kujifunza namna wenzetu wanavyoendesha ratiba zao Kwa mafanikio bila kuwa na longolongo ya viporo. Tumeona Ligi Kuu England bingwa amepatikana mchezo wa mwisho na wote walipambana mwanzo mwisho kuwania ubingwa jambo linaloongeza thamani ya ligi pamoja na ushindani.

 

Wenzentu pia wana mashindano mengi kama Ligi ya Mabingwa Ulaya, FA na Carabao, lakini bado wamefanikiwa msimu kwa wakati bila longolongo, je, sisi tunakwama wapi? Tunatakiwa kujiuliza mapema. Mpaka sasa ligi inakaribia kufika ukingoni bado kuna timu zina viporo, hili linapaswa liangaliwe kwa ukaribu msimu ujao haya yasiwepo na yatafutiwe dawa kabisa.

Timu zote zinazoshiriki ligi zinapaswa kujipanga na kupambana kwa hali na mali kupata matokeo chanya huku Bodi ya Ligi Tanzania ikitazama namna ya kuwa na ratiba bora itakayoleta ushindani.

 

Wengi tunapenda kuona ligi ya ushindani kama mwanzo ilivyoanza kila timu ilipambana kupata matokeo na hakukuwa na matatizo mengi kama sasa hasa mzunguko wa pili. Malalamiko mengi ambayo yanatokea kwa sasa ni kwa timu nyingi kuona zinaonewa hasa na maamuzi ya waamuzi pamoja na kampeni zilizopo ugenini, hii inavunja ushindani. Wimbo wa waamuzi umekuwa ukiimbwa sana nina imani Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) litafanyia kazi haya na kuwachukulia hatua wale wote ambao wanashindwa kutimiza majukumu yao kwa usahihi.

 

Pia ingependeza kama hatua zitachukuliwa baada ya muda mfupi kama ilivyokuwa kwenye mchezo wa Simba na KMC itaongeza heshima kwenye ligi. Lala salama huwa si muda rafiki kwa timu ambazo zina hatihati ya kushuka daraja, kila mmoja anapambana kutafuta matokeo hivyo michezo mingine inayochezwa ni ya maajabu.

 

Suala la mdhamini ambalo msimu huu unakamilika likiwa bado halijaeleweka ni muhimu kutafutiwa ufumbuzi ili kupunguza ule ugumu wa kuendesha timu ambao ulikuwa unazikabili timu nyingi.

 

Haikwepeki kwamba ligi yetu ilipoteza mvuto mwishoni kutokana na timu nyingi kuyumba na kufanya wengi wabuni mbinu mbadala kujikwamua kiuchumi hasa kwenye suala la uendeshaji wa ligi. Kwa sasa Bodi ya Ligi inapaswa ianze michakato mapema ya kutafuta mdhamini maana waliahidi kwamba msimu huu mambo yatakwenda kama yalivyoanza ila msimu ujao kuna kampuni kubwa itawekeza kutoka Afrika Kusini.

 

Ni ngumu sana kuwaamini wanasiasa kotokana na sera zao kuwa za kufikirika ila nina amini kwenye michezo hakuna masuala ya siasa hivyo wengi tuna imani kwamba msimu wa kesho kila kitu kitakuwa sawa.
Pia kama mambo yatakuwa kombo ni vema timu zikaambiwa mapema kuliko kuwashtukiza ligi inaanza na wenyewe wana imani ya kupata mdhamini mambo yanakuwa ndivyo sivyo.

 

Kila timu ambayo ipo ligi kuu pia inapaswa ijiandae kisaikolojia namna ya kukabili changamoto ambazo wamezipitia msimu huu kwa ajili ya kufanya vizuri msimu ujao. Wengi wana hasira za kuonewa na ugumu wa lgi ulivyo hasa kwenye masuala ya kiuchumi ila hamna namna yote ni lazima yatokee ila kikubwa safari ya mafanikio ya soka lazima iendelee. Rai yangu msimu ujao waamuzi wapewe somo na kanuni za kuzingatia pia wapewe waangalizi wengine mbadala ambao watasaidia kupunguza lawama kwani wanazidi kudamaza maendeleo ya soka letu. Muda uliopo wa kutafuta mafanikio ni sasa hivyo tunapaswa tujipange kupambana kuyatafuta mafanikio kwani tuna safari ndefu kwa sasa.

 

MAMBO yanazidi kuwa mengi kwa sasa hasa ukizingatia Ligi Kuu Bara inaelekea ukingoni na kila timu inapambana kupata matokeo chanya kwenye michezo yake iliyobaki. Tunaona mpaka sasa bado mbio za ubingwa zimeachwa mikononi mwa vigogo wawili ambao ni Simba na Yanga, huku wengine wakinyoosha mikono mapema na kuhamishia ushindani sehemu nyingine kama kubaki tano bora na wengine wanapambana kutoshuka daraja. Mengi ambayo kwa sasa yanatokea ni matokeo ya maandalizi ya timu kwa ujumla kwenye michezo yao pamoja na hali halisi ya soka letu la Tanzania, hakuna namna nyingine ya kusema. Ratiba zimekuwa zikizibana timu nyingi kutokana na mpangilio usioridhisha kwa timu nyingi huku baadhi zikipewa kipaumbele hali inayosababisha kuwe na viporo vingi.
Selemani

Comments are closed.