Yametimia! Hivyo ndivyo unavyoweza kusema kufuatia kukabidhiwa zawadi kwa washindi wa droo za mwisho za Shindano la Tusua Maisha, zoezi lililoenda sambamba na uzinduzi wa Gazeti la Spoti Extra Toleo la Ahamisi.
Mpango mzima ulikuwa ni kwenye Uwanja wa Bakhresa, Manzese jijini Dar es Salaam ambapo washindi waliokuwa wakisubiri kwa hamu zawadi zao, walikabidhiwa na hivyo kumalizika rasmi kwa Shindano la Tusua Maisha na Global lakini pia kuanza kwa shindano lingine ndani ya Gazeti la Spoti Extra.
Waliokabidhiwa zawadi zao ni Bholen Kilimba wa Tukuyu, Mbeya aliyefunga safari kutoka Mbeya mpaka Dar es Salaam kupokea zawadi yake ya pikipiki mpya, Halima Jabir wa Mbagala aliyesindikizwa na wazazi wake kupokea pikipiki yake na Hamis Mohamed wa Kinondoni aliyeondoka na dinner set.
Wengine ni Vaileth Mtilega wa Kiwalani aliyeondoka na jezi na Eliuter Ndunguru wa Manyoni aliyewakilishwa na Odilia Ndunguru kupokea jezi zake.
Burudani mbalimbali zilipamba tukio hilo lililokusanya umati mkubwa ambapo pia wasomaji wa Gazeti la Spoti Extra walipata bahati ya kujishindia zawadi mbalimbali za papo hapo kutokana na kujaza kuponi zilizopo ndani ya gazeti hilo, ambalo sasa litakuwa likitoka mara mbili kwa wiki, Alhamisi na Jumapili kwa bei ya shilingi 500 tu.
Kabla ya tukio hilo, asubuhi ya leo, Septemba 20, viongozi mbalimbali na wafanyakazi wa Kampuni ya Global Publishers waliingia mitaani kuuza gazeti jipya la Spoti Extra Toleo la Alhamisi lililopokelewa kwa kishindo na wasomaji wake, nchi nzima.
Comments are closed.