The House of Favourite Newspapers

VYAKULA VINAVYOSAIDIA KUPUNGUZA UZITO/UNENE !

MOJA kati ya matatizo yanayowakumba watu wengi kwa kizazi cha sasa ni tatizo la uzito. Tatizo hili limekuwa chanzo cha matatizo mengine makubwa na yenye madhara makubwa kwa afya ambayo wakati mwingine husababisha kifo.

Magonjwa ya moyo, kisukari, shinikio la damu la kupanda na kushuka, matatizo ya figo na viungo vingine vya mwili pamoja na kukosa mvuto wa kawaida yanasabishwa na mtu kuwa na uzito ambao anashindwa kuumudu.

Uzito huongezeka kutokana na mtindo fulani wa maisha ya mwanadamu hasa kwenye chakula. Ifuatayo ni orodha ya vyakula vya aina nne tofauti ambavyo vinasaidia sana kupungua uzito.

MAYAI

Katika miaka ya hivi karibuni tafiti nyingi ambazo si sahihi na si za kweli zimesababisha watu kutozingatia ulaji wa mayai hasa ile sehemu ya kiini cha yai, watu wengi wameaminishwa kuwa kiini cha yai kina mafuta ambayo ulaji wake huweza kufanya mtu anenepe bila mpangilio.

Mafuta yanayopatikana kwenye kiini cha yai si mafuta mabaya bali ni yale ambayo mwili unayahitaji na hayana hatari kwa mwili wa binadamu.

CHOKOLETI YA KAHAWIA

Si kila chokoleti zina madhara kwa mwanadamu na baadhi yake ikiwemo zile za kahawia zina faida kubwa mwilini. Asilimia 70 ya chembechembe zinazotengeneza chokoleti ya kahawia ni kokoa, chokoleti hii ina virutubisho pamoja na madini muhimu mwilini kama vile Magnesium pamoja na manganese ambayo husaidia mwili katika masuala mbalimbali ikiwemo kuponya vidonda na kurudishia chembechembe hai za mwili zinazopotea.

Chokoleti ya kahawia pia husaidia kupunguza uwezekano wa mtu kupata maradhi ya moyo na maradhi mengine yatokanayo na shinikizo la damu na pia hainenepeshi.

SAMAKI DAGAA

Samaki wadogo ambao hufahamika kama dagaa wana faida nyingi sana mwilini, kwani huliwa nyama yake pamoja na ngozi yao, mifupa na vitu vyote vilivyomo ndani yake ambavyo kimsingi vina faida kubwa sana mwilini.

Dagaa wana virutubisho ambavyo mwili wa mwanadamu unahitaji na vinaboresha afya na kumpa mtu nguvu pamoja na kinga dhidi ya magonjwa na pia kusaidia kuponya magonjwa pale mtu anapokuwa mgonjwa na hufanya mwili usinenepe.

NYAMA YA INI

Nyama nyekundu zina madhara makubwa zinapoliwa kwa wingi na pasipo mpangilio. Lakini nyama ya ini ambayo ina virutubisho muhimu kama vile Vitamin A, madini mbalimbali kama Shaba, Zinc, Selenium, Folate na Niacin pamoja na Protini kwa kiwango kikubwa na virutubisho vyote hivi vina faida kubwa sana mwilini kwani hainenepeshi, kula nyama ya ini kila mara.

Comments are closed.