Waziri Mkuu: Dkt. Samia Ni Rais Wa Vitendo, Ametoa Ajira mpya 12,000

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Rais wa vitendo na amethibitisha hayo katika kipindi alichoingoza Tanzania kwa kuboresha miundombinu kwenye sekta mbalimbali.
Amesema mafanikio makubwa yamepatikana chini ya uongozi wake wa miaka minne na nusu ikiwemo ujenzi wa hospitali 119 katika wilaya zisizo na hospitali, vituo vya afya 640 katika kata za kimkakati na tarafa, zahanati zaidi ya 800 vijijini pamoja na ujenzi wa shule mpya za msingi zaidi ya 2,700.
“Amejenga shule za sekondari zaidi ya 1,300 na madarasa 79,000 katika maeneo yaliyokuwa na uhitaji wa madarasa. Haya yamesaidia kuondoa tatizo la wanafunzi kusubiri kujiunga na sekondari kwa sababu ya uhaba wa madarasa. Hatua hii imemaliza utaratibu wa uchangishwaji kwa nguvu na kamatakamata za ujenzi wa vyumba vya madarasa,” amesema.

Akielezea kuhusu utendaji kazi wa Rais, Waziri Mkuu amesema ujenzi wa miundombinu bora ya elimu na afya iliyojengwa na Serikali, inahitaji watumishi wa kutosha na ndiyo maana Rais ametoa msukumo wa haraka kwenye ajira hizo na ndiyo maana aliahidi maeneo 13 ya vipaumbele ndani ya siku 100 tangu ashike madaraka.
Dkt. Mwigulu amesema ili kutekeleza ahadi za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia, Serikali imeidhinisha ajira mpya 12,000 zikijumuisha 5,000 za kada ya afya na 7,000 za sekta ya elimu ambapo usaili utaanza Desemba 10, 2025 katika kila mkoa na watumishi hao wataanza kuripoti vituoni kuanzia Januari 10, 2026 hatua ambayo itaimarisha zaidi utoaji wa huduma nchini. “Nia ya Serikali ni kufanya vituo vya afya na shule zetu zipate watumishi,” amesisitiza.
Amesema kuwa Rais Samia ametekeleza mambo makubwa katika maboresho ya mifumo ya kijamii ikiwemo kuanza utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote ambapo makundi ya watoto, wazee na wajawazito ndiyo yatakuwa ya kwanza kunufaika.

