The House of Favourite Newspapers

Wiki ya Mwananchi kuweka historia Yanga

MWENYEKITI wa Kamati ya Wiki ya Mwananchi, David Ruhango, ameahidi kuandika historia mpya ya soka nchini kwa kufanya tukio kubwa siku hiyo ya kilele ambayo ni Agosti 4, mwaka huu.

 

Tukio hilo kubwa litakalokuwa la kihistoria limepangwa kufanyika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kwa timu hiyo kucheza mchezo wake wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Kariobangi Sharks ya nchini Kenya.

 

Katika siku hiyo ya kilele Yanga, imepanga kutambulisha kikosi chao kipya watakachokitumia msimu ujao. Ruhango alisema kabla ya kilele cha Wiki ya Mwananchi yapo matukio mengi wamepanga kufanya ikiwemo la awali la kwenda kutoa misaada hospitalini na kufanya usafi kwenye maeneo mbalimbali ya nchini wakiwashirikisha mashabiki wao.

 

“Siku hiyo ya kilele tumepanga kufanya matukio mengine makubwa ambayo yatakuwa ‘surprise’ siku hiyo ya kilele ya Wiki ya Mwananchi, hivyo Wanayanga wajitokeze kwa wingi uwanjani kushuhudia matukio mbalimbali,” alisema Ruhango na kuongeza: “Tunafahamu Wanayanga wana kiu ya kukiona kikosi chao kipya, hivyo ni siku yao maalum kujitokeza kwa wingi uwanjani kwa ajili ya kuangalia usajili wa wachezaji wetu ambao watatumika kwa ajili ya msimu ujao.”

Comments are closed.