The House of Favourite Newspapers

Yondani afichua usajili mpya Yanga

Kelvin Yondani

BEKI mkongwe wa kati wa Yanga, Kelvin Yondani amesema kuwa kikosi hicho kinahitaji mastraika, mabeki wa kati na kipa imara. Mchezaji huyo mzoefu amesisitiza kuwa hajaona tatizo lolote kwenye safu ya kiungo cha timu hiyo msimu huu.

 

Safu ya ushambuliaji wa Yanga inaongozwa na Mkongomani, Heritier Makambo, Amissi Tambwe, Ibrahim Ajibu huku ulinzi ikiundwa na Andrew Vicent ‘Dante’, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na yeye mwenyewe.

 

Akizungumza na Spoti Xtra, Yondani alisema ni ngumu kupata ushindi katika mechi kwa kumtegemea mshambuliaji mmoja pekee ambaye ni Makambo na badala yake timu yao inahitaji kusajili washambuliaji wengine wenye uwezo na uzoefu wa kucheza mashindano mbalimbali.

 

“Timu yetu inahitaji maboresho madogo ya kikosi kwa kuanza ni kusajili washambuliaji wa kati, mabeki wa kati na kipa ambao wote wenye uzoefu wa kuamua mechi.

 

“Ukiangalia hivi sasa katika timu mshambuliaji tunayemtegemea ni mmoja pekee ambaye ni Makambo, kama siku ikitokea akawekea ulinzi mkali, basi timu inakuwa ni vigumu kupata matokeo, hivyo ni lazima tusajili washambuliaji kama kweli tunataka ubingwa msimu ujao,”alisema Yondani ambaye aliwahi kuichezea Simba.

 

“Pia, kipa anahitajika yule mwenye uwezo na uzoefu kwa sababu kama mabeki wakiwa wazuri halafu kipa hakawa hana uwezo ni lazima tutafungwa,”alisisitiza Yondani ambaye ana mjengo Kigamboni. Kati ya wachezaji wanaowindwa na Yanga ni kipa Farouk Shikalo wa Bandari ya Kenya.

 

Mchezaji huyo tegemeo wa Taifa Stars aliongeza kuwa; “Safu ya kiungo binafsi naona hakuna haja kusajili wengine kwani tayari wapo Fei Toto (Feisal Salim), Banka (Issa Mohamed), Bobani (Haruna Moshi)  na Tshishimbi (Papy) wote wapo vizuri.”

 

WILBERT MOLANDI,    Dar es Salaam

Comments are closed.