The House of Favourite Newspapers

Niyonzima Aifuata Simba Afrika Kusini ‘Sauz’

0
Kiungo mpya wa Simba, Mnyarwanda, Haruna Niyonzima.

KIUNGO mpya wa Simba, Mnyarwanda, Haruna Niyonzima, aliyesajiliwa akitokea Yanga, kwa mara ya kwanza ataungana na nyota wenzake wa timu hiyo, Julai 29, mwaka huu katika kambi ya timu hiyo nchini Afrika Kusini ‘Sauz’.

Niyonzima ametua Simba baada ya kumalizana na Yanga ambapo amemaliza mkataba huku pia klabu yake hiyo ya zamani ikiweka bayana kuwa haitaendelea naye kwa msimu ujao baada ya kushindwana kwenye masuala ya maslahi.

Simba kwa sasa wamejichimbia Sauz ambako wanaendelea na kambi yao ya siku 20 wakijiandaa na msimu ujao ambapo wanatarajiwa kurejea Agosti 6, mwaka huu kwa ajili ya siku ya Simba Day ambayo itafanyika Agosti 8, mwaka huu.

Haruna Niyonzima akiweka sawa kamba zake.

Chanzo cha ndani ya Simba kimeliambia Championi Jumatano kuwa, Niyonzima aliyetokea APR ya kwao Rwanda kabla ya kutua Yanga, atatua Sauz kuungana na wenzake siku hiyo baada ya siku zake za kimkataba na Yanga kumalizika.

“Kwa mara ya kwanza Niyonzima atavaa jezi za Simba Julai 29, mwaka huu ambapo ataungana na wenzake nchini Afrika Kusini ambapo kikosi kimepiga kambi ya siku 20 ya kujiandaa na michuano mbalimbali kwa msimu ujao, ambapo rasmi mkataba wake na Yanga utakuwa umefika ukingoni.

“Lakini mashabiki wengi watamuona siku ya Simba (Simba Day) Agosti 8, mwaka huu ambapo ndiyo atatambulishwa rasmi kwao sambamba na nyota wengine ambao tumewasajili hivi karibuni,” kilisema chanzo hicho.

Inaelezwa Haruna Niyonzima ameshasaini mkataba wa miaka miwili Simba kwa dau la dola 50,000 ambazo ni zaidi ya Sh milioni 110 za Tanzania. Lakini Simba wanavizia mkataba wake Yanga uishe kabla ya kumtangaza kwa kuhofia adhabu ya kumsainisha mkataba akiwa ndani ya mkataba.

Stori: Said Ally | Championi Jumatano | Dar es Salaam

Leave A Reply