Enock Bella wa Ya Moto Band akiwa ametulia nyumbani.
MAMBO vipi mpenzi msomaji wangu, leo katika safu yetu hii tunaye Enock Bella ambaye ni mmoja wa memba wa Ya Moto Band anayezidi kujizolea umaarufu mkubwa kutokana na sauti yake ya besi huku mwenyewe akiwa na umri mdogo pamoja na mwili mdogo.
Mpaka Home ilitinga mpaka kwenye kambi ya Mkubwa na Wanawe iliyopo Temeke Mwembe Yanga anakoishi mkali huyo, kujua mengi zaidi twende pamoja:
Maisha yake ya kila siku yakoje?
“Maisha yangu ni ya kawaida sana napenda kujichangaya na watu sipendi kujitenga na sipendi pia kujionesha mimi ni nani na kuna wakati mtu anaweza hata asinijue.”
Ni sehemu gani anapenda kukaa anapotunga nyimbo?
“Sehemu ambayo nikikaa nakuwa na imani moyoni wangu ni chumbani huko nakuwa natuliza akili kwa sababu nakuwa najifunza vitu vingi sana kwa kufikiria kwa sababu nakuwa napata akili ya kubuni vitu vingi ambayo naamini kabisa vitaniletea mafanikio.”
Alishawahi kupika au kuosha vyombo?
“Hilo ni jambo la kawaida sana kwa sisi mabachela kwa sababu utakula vibandani mwisho wa siku utachoka hivyo siku zingine inakubidi ujipikie na ukishamaliza kula inabidi uoshe vyombo vyako, huwezi kuviacha vikiwa vichafu.”
Vipi kutandika kitanda kwake siyo ishu?
“Najua kabisa wanaume wengi hasa vijana kama sisi mageto yanakuwa siyo lakini nafikiri wewe (Mpaka Home) ni shahidi umeona geto langu liko vizuri na huwezi amini cha kwanza kabisa nikiamka kutoka kitandani ni kuweka kitanda changu safi na nina kitandika utafikiri kuna mdada ndani anafanya kazi hiyo.”
“Aisee bado, kwanza umri wangu mdogo, pia nahitaji kupanga maisha ili niweze kuilea hiyo familia yangu ya baadaye lakini kwa sasa no!”
Nini siri ya sauti yake nene?
“Hizi ni kudra tu za Mwenyezi Mungu kunijalia sauti kama hii ambayo ndiyo imekuwa kivutio kikubwa sana na hapo mwanzo nilijiona kama sifai lakini mkubwa alivyoisikia alisema kuwa hiyohiyo ndiyo itatumika nikashukuru sana.”
Ratiba yake ya siku nzima ikoje?
“Mara nyingi naamka saa nne asubuhi, napenda kufungua kinywa na juisi pamoja na chapati, sipendi chai. Kisha najifungia ndani kuanza kujifunza ‘biti’ mbalimbali kwa sababu napenda kuja kuwa prodyuza. Unapofika muda wa msosi, nakula kisha naingia kwenye mazoezi nikimaliza naendelea kujifunza kutengeneza biti mpaka usiku ninapolala.”
Faida gani amezipata kutokana na muziki?
“Ni nyingi sana nimeweza kujuana na watu na nimeweza kusafiri nchi mbalimbali kwa kupitia muziki ninaofanya.”
