
Thomas Ulimwengu
Sweetbert Lukonge | CHAMPIONI, Dar es Salaam
MAMBO yanamwendea vizuri straika wa Tanzania, Thomas Ulimwengu katika kikosi cha AFC Eskilstuna kinachoshiriki Ligi Kuu ya Sweden, kwani licha ya kuanza mazoezi, timu hiyo imemuombea Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) mchezaji huyo.
Siku chache tu baada ya kuanza mazoezi na timu hiyo, timu hiyo imetuma barua kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ikiomba ITC ya Ulimwengu ili aweze kujiunga nao, hii inamaanisha klabu hiyo imekoshwa na uwezo wa straika huyo.
Ulimwengu ambaye alikuwa akiichezea TP Mazembe ya DR Congo, alijiunga na timu hiyo Jumatatu ya wiki hii na kuanza mazoezi juzi Jumatano kwa mujibu wa Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas.
Ofisa Habari wa TFF, Alfred aliliambia Championi Jumamosi kuwa, AFC Eskilstuna imetuma maombi ya ITC ya Ulimwengu jana na leo hii wanatarajia kuituma ili akaanze kazi yake ya kucheza soka mara moja.
“Leo hii (jana) tumepokea maombi ya ITC ya Ulimwengu kutoka AFC Eskilstuna na hivi sasa tupo katika harakati za kuiandaa hivyo mpaka kufikia kesho (leo) itakuwa tayari tumeituma,” alisema Alfred.
Ulimwengu amesaini mkataba wa miaka miwili na klabu hiyo.