
ILE droo ndogo ya tano ya shindano la Bahati Nasibu la Shinda Nyumba linaloendeshwa na Kampuni ya Global Publishers kupitia Magazeti ya Championi, Ijumaa, Ijumaa Wikienda, Risasi, Risasi Mchanganyiko, Amani na Uwazi imefanyika leo Alhamisi Julai 20, katika Viwanja vya Las Vegas vilivyopo Mabibo jijini Dar es Salaam.

Katika droo hiyo, Geofrey Shangalawe (53) Mkazi wa Kigoma ameibuka mshindi wa Televisheni ‘flat screen’ mpya ambapo baada ya kupigiwa simu na MC Chaku aliyekuwa akiendesha droo hiyo, mshindi huyo hakuamini mara moja kama kweli ameshindia flat screen.

“Aaaaaa, aisee! TV nchi ngapi? Hahahaaa! Sina hata la kusema, mwanzoni nilidhani washindi wanapangwa tu, lakini kumbe siyo, siamini kama nimeshinda, nawashukuru sana Global. Niwaombe na wasomaji wengine wasikate tamaa maana hata mimi sikujua kama nitashinda siku moja,” alisema Shangalawe kwa njia ya simu.


Washindi wengine waliopatikana katika droo hiyo ni pamoja na Festo Masagasi mkazi wa Bunju jijini Dar aliyejishindia Smart Phone mpya aina ya Tecno, Salome Msaru wa Mtwara na Ummysalama Sasha wa Dar ambao wote waliibuka washindi wa vyombo vya nyumbani (dinner set).

Mwingine ni Anthony Thomas mkazi wa Mabibo jijini dar aliyejishindia fulana mpya ya shinda nyumba.

Kutokana uwazi uliofanyika katika zoezi zima la uchezeshwaji wa bahati nasibu hiyo hata alipotajwa mshindi wa mwisho umati huo ulionekana kushangilia na kuyakubali matokeo hayo huku wengine wakiahidi kuzidi kushiriki mchezo huo ambapo siku ya mwisho mshindi ataibuka na nyumba mpya yenye fenicha zote ndani.

Shindano hilo linadhaminiwa na King’amuzi cha Ting, British Schools pamoja na Kampuni ya Simu za mkononi ya Tecno.


PICHA NA RICHARD BUKOS | GLOBAL TV ONLINE