




TIMU ya wafanyabiashara wa Korea na Tanzania waliopitisha mkataba wa kushirikiana, wakiongozwa na mratibu wa timu hiyo, diwani na mwenyekiti mstaafu wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema, Mathew Lubongeja, ambaye kwa sasa yuko nchini Korea, walimtembelea Balozi wa Tanzania nchini humo, Matilda John Masuka.
Wafanyabiashara hao ni wa kampuni mbili za Tanzania ambazo ni Blue Mark iliyo chini ya Mkurugenzi wake, Eric Shigongo, na JONTA Investment Ltd iliyo chini ya Mkurugenzi John Elias Ntalimbo wa Shinyanga. Kampuni hizo zimesaini mkataba wa kuungana na kufanya kazi na kampuni ya Sungwoo I. D. Construction Co. Ltd ya Korea ya Kusini inayoongozwa na Jeun Ki Wook ambapo mkataba huo unahusu ushirikiano katika kukuza sekta ya ujenzi.
Kabla ya kumtembelea balozi huyo, wafanyabiashara hao walikuwa na mkutano uliofikia makubaliano ya ushirikiano wa kimaendeleo baina ya mji wa Sengerema, mkoani Mwanza, na Jiji la Gyeongsan la Korea Kusini.