
MABOSI wa Simba tayari wamekubaliana kumpa mkataba beki Muivory Coast, Pascal Serge Wawa kwa sharti la kufanya vipimo kabla ya kumsainisha ili kujua afya yake, lakini wakitaka afanye kazi tatu kwa wakati mmoja.
Hiyo ikiwa ni siku chache tangu beki huyo atue hapa nchini na kuanza mazoezi ya pamoja na Simba katika kujiandaa na Kombe la Kagame litakalofanyika jijini Dar es Salaam, kuanzia keshokutwa Ijumaa.
Beki huyo juzi Jumatatu asubuhi alianza kufanya mazoezi kwenye Uwanja wa Boko Veterani, Dar huku akiwa na Mnigeria, Victor Patrick.
Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatano, Simba wamefanya mazungumzo na beki huyo na kufikia muafaka wa kumsajili kwa dau la shilingi milioni 30 kwa mkataba wa mwaka mmoja pekee.
Mtoa taarifa huyo alisema, uongozi bado una hofu na afya yake, ndiyo maana usajili wake utafanyika mara baada ya kufanyiwa vipimo.
“Wawa mkataba wake ulimalizika El Mareikh tangu Desemba, mwaka jana na alikaa nje kwa muda wa takriban miezi sita bila ya kuwa na timu, hivyo kuna wasiwasi na afya yake anaweza kuwa majeruhi.
“Atafanyiwa vipimo kwanza ambapo vipimo hivyo vitafanyika leo (jana Jumanne) na kama ikionekana hana majeraha yoyote basi atasaini mkataba kwani tayari tumefikia makubaliano hayo ya kumsajili kwa mkataba wa mwaka mmoja.
“Tumefikia uamuzi wa kumchukua Wawa kwa sababu anapokuwa uwanjani atatakiwa kufanya kazi nyingi, kwanza kiongozi kwa wenzake, pia atakuwa mwalimu lakini pia tunajua atatumia uwezo wake kupambana na washambuliaji wakali,” alisema mtoa taarifa huyo.
Championi lilizungumza na Wawa na kusema: “Ni kweli bado sijasaini mkataba, tupo kwenye mazungumzo mazuri na Simba na kama mambo yakikaa sawa basi nitasaini mkataba.”
Stori: Wilbert Molandi, Dar es Salaam
