×

Yondani Mambo Safi Yanga SC

BEKI wa kati wa Yanga, Kelvin Yondani ambaye kila siku ya Mungu anavuka maji ya Bahari ya Hindi kuelekea kwake Kigamboni, usajili wake wa mkataba wa miaka miwili umekwangua karibu nusu ya mapato ya mlangoni ya klabu hiyo ya msimu uliopita.

Yondani ambaye amekuwa hana mpinzani Jangwani, amesaini kwa Sh milioni 60. Mwenyekiti wa zamani wa Yanga, Tarimba Abbas ambaye pia ni Mku­rugenzi wa Utawala na Utekelezaji wa Kampuni ya Sportpesa Tanzania ndiye aliyepewa jukumu la kuhak­ikisha beki huyo anabaki Yanga kwa kumsajili pamoja na Hassani Kessy.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumamosi kutoka kwa bosi mkubwa mwenye ushawishi wa usajili, beki huyo ali­saini mkataba huo jana Ijumaa ikiwa ni baada ya kumaliziwa nusu ya fedha za usajili alizoahidiwa.

“Yondani amesaini mkataba wa miaka mingine miwili ya kuendelea kuichezea Yanga na mechi ijayo ya marudiano atakuwepo kikosini kui­pambania timu yake.

“Hivyo, bosi huyo hivi sasa ameha­mia kwa Kessy ambaye naye tayari alifanya naye mazungumzo na kutaja dau la shilingi milioni 50 analolihitaji ili asaini mkataba wa kubaki Yanga,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Alipotafutwa Tarimba kuzungumzia hilo alisema kuwa: “Asilimia 100 Yon­dani anabaki kuichezea Yanga katika msimu ujao wa ligi, hiyo ni baada ya kufikia muafaka mzuri wa kusaini kati yangu na baadhi ya mashabiki wa Yanga wenye mapenzi mema na klabu yao.

“Kiukweli niwashukuru baadhi ya watu waliofanikisha usajili wa Yon­dani Yanga ambaye kwenye msimu ujao tutakuwa naye ambao ni kundi la WhaatsAp la Yanga Viva na mtu mmoja ambaye ni shabiki mwenye mapenzi na timu yake, jina lake maarufu ni Yanga Makaza anayeishi mkoani Mwanza.

 

“Pia nimshukuru Yondani mwenyewe ambaye ni muhimili mkubwa katika timu kwa kufanikisha usajili wake pamoja na kaka yake, Sunday ambaye ni meneja wake bila kuisahau familia ya Yondani am­bayo imefanikisha kubakia, hivi sasa ninaelekeza nguvu kwa Kessy ambaye naye nilifanya naye mazungumzo am­bayo yamefikia pazuri wakati wowote tutalimaliza hilo,” alisema Tarimba.

Wilbert Molandi, Dar es Salaam.