
Bibi mmoja aliyefahamika kwa jina la Rehema Shabani mkazi wa Kulangwa, Tegeta ‘A’ jijini Dar, hivi karibuni nusura afariki dunia baada ya kuzimia kwa muda mrefu alipokuwa akimlilia Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi kisa kikiwa ni tishio la nyumba yake kubomolewa.
Tukio hilo lililosababisha wajukuu zake waanze kulia wakidhani tayari wamempoteza bibi yao lilitokea juzi wakati bibi huyo akiongea na waandishi juu ya tishio la nyumba yake aliyoijenga kwa kudunduliza kubomolewa baada ya kuandikwa ubavuni ‘simamisha ujenzi’.
Akizungumza kwenye mkutuano uliowakutanisha wakazi takribani 100 wa eneo hilo uliofanyika Jumapili iliyopita, Bi. Rehema alisema kuwa, awali alikuwa akiishi Morogoro lakini miaka ya nyuma kidogo nyumba yake ilibomolewa kupisha ujenzi wa reli ambapo aliamua kuja Dar es Salaam.
“Nilikuwa nikiishi Morogoro, sasa eneo nililokuwa naishi serikali ilisema tumejenga katika eneo la ujenzi wa reli, kibanda changu kikabomolewa. “Nikajichangachanga kwa biashara yangu ya vitumbua na uzee huu, nikapata pesa na kuja kujenga hapa angalau nijisitiri.
“Sasa juzi nimetoka nje nakuta nyumba yangu ambayo tayari naishi imeandikwa simamisha ujenzi. Nilichanganyikwa, nikawa najiuliza walioandika maneno hayo ni nani. Ndipo jirani yangu mmoja akaniambia ukiona umeandikiwa hivyo ujue itabomolewa.
“Hapo ndipo nilipopata presha. Morogoro nimebomolewa, hapa napo jamani…. naumia sana. Namuomba Waziri Lukuvi anisaidie,” alisema bibi huyo huku akilia. Wakati akiendelea kutoa maelezo huku akilia, ghafla bibi huyo alitulia na kuonekana aliyeishiwa nguvu, akaanguka na kupoteza fahamu hali iliyosababisha mkutano kusimama kwa muda.

Wasamaria wema waliokuwa eneo la tukio walilazimika kumpepea ili kumzindua lakini ilichukua muda mrefu, ambapo wajukuu zake walianza kulia wakihisi bibi yao amewatoka. Hata hivyo baadaye alizinduka na kufanya mkutano huo uendelea ambapo muwakilishi wa wananchi hao, Venance Mpihigwa alisema kuwa, awali eneo hilo lilikuwa na mgogoro kati ya wananchi na familia ya mtu aliyefahamika kwa jina la Seif Ngane lakini Mkuu wa Wilaya ya Ubungo alifika na kuumaliza mgogoro huo kisha kuwaamuru wananchi kuendelea kujenga kwa kuwa walikuwa na uhalali wa umiliki.
“Sisi tuko eneo hili kihalali kabisa na tunamshukuru sana Mkuu wa Wilaya ya Ubungo ambaye kuna wakati alifika eneo la tukio ikiwepo familia ya Ngane iliyokuwa ikidai eneo hilo ni lao lakini mwisho kwa vielelezo vilivyopo visivyo na makengeza, aliamuru wananchi waendeleze makazi hayo.
“Cha ajabu sasa kuna watu kutoka Manispaa ya Ubungo ambao bado wamekuwa wakituletea usumbufu akiwemo Mrando (Afisa Ardhi Ubungo). Usumbufu huo ulitulazimu tufanye jitihada za kutaka kumuona Waziri Lukuvi ili ajue kwamba kuna watendaji wake huku chini wanasumbua raia.
“Lakini sasa wakati tukifanya jitihada za kumuona Lukuvi, juzi kuna gari ilikuja ikiwa na polisi wawili na watu wengine kama 8 hivi, wakaanza kuchora nyumba za raia kwamba wasimamishe ujenzi. Nyumba takribani 40 zimechorwa.
“Jambo hilo lilizua taharuki kubwa sana, lingekuwa ni zoezi lililofuata utaratibu isingekuwa tatizo lakini watu ambao hawajulikani, kufika kwenye makazi ya watu na kuanza kuandika, huoni inaweza kuleta uvunjifu wa amani?
“Tumejaribu kwenda kuuliza Manispaa ya Ubungo kujua kama kuna watu wamewatuma kufanya hivyo na kwa sababu zipi lakini hakukuwa na majibu ya kueleweka. Wananchi wako njia panda. Kwa hiyo tunamuomba Waziri Lukuvi ajue kuna tatizo katika eneo letu na ikibidi afike kwani akichelewa kuna siku damu itamwagika,” alisema kiongozi huyo.

Naye Benitho Chiwinga ambaye nyumba yake imeandikwa ‘SIMAMISHA UJENZI’ alisema: “Kuna mambo ya ajabu sana yanafanyika huku na ni vyema Lukuvi akajua. Hivi ‘from no where’ unakuta nyumba ambayo umeihangaikia kwa muda mrefu, leo anakuja mtu na kuandika bomoa kienyeji tu, haya yanawezaje kufanyika kwenye nchi hii inayoongozwa na rais anayetetea wanyonge? Lukuvi njoo Tegeta A, Kulangwa. Watendaji wa Manispaa ya Ubungo wanakuharibia kazi.”
Mwandishi wetu ambaye alikuwa eneo la tukio Jumapili iliyopita alishuhudia wananchi wengi wakiwa mtaani na mabango yaliyoandikwa; ‘RAIS MAGUFULI, SISI WANYONGE WA KULANGWA TEGETA ‘A’ TUNANYASIKA, TUSAIDIE.
Lingine liliandikwa; MAKONDA NJOO KULANGWA UTUSAIDIE BABA. Lingine lilikuwa na maneno haya: WAZIRI LUKUVI, WATENDAJI MANISPAA YA UBUNGO WANAKUHARIBIA KAZI, NJOO TEGETA ‘A’ TUNAONEWA! Aidha, mwandishi wetu pia alipata fursa ya kuziona nyumba hizo zipatazo 42 zikiwa zimeandikwa ubavuni maneno ya SIMAMISHA UJENZI wakati zimeshakamilika na watu wanaishi.
Stori: MWANDISHI WETU, Dar
