




wafanyabiashara Pemba.


MKUU wa Wilaya ya Chake Chake Rashid Hadid Rashid, amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, inaunga mkono juhudi mbali mbali zinazochukuliwa na benki ya NMB, katika kuwaunganisha wafanyabiashara wa Kisiwa cha Pemba, jambo linaloweza kupelekea kuongezeka kwa mapato ya nchi.
Alisema wafanyabiashara ni watu muhimu katika maendeleo ya uchumi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla, katika suala zima la kukusanya mapato.
Alisema malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuhakikisha, inaboresha mapato ya serikali kupitia kodi na kuziba mianya yote ya ukwepaji wa kodi, ambayo husababisha upotevu wa mapato ya serikali hali inayopelekea kuzoretesha maendeleo ya nchi.
Mkuu huyo wa Wilaya ya aliyaeleza hayo, mjini chake chake wakati wa uzinduzi wa klabu ya wafanyabiashara wa Pemba, ikiwa ni klabu ya kwanza kisiwani hapa kuanzishwa na NMB.
“Muunganiko huu pia utaweza kutoa mafunzo kwa wafanyabiashara, katika suala la kodi na jinsi ya kutunza fedha, jambo hili ni muhimu litaweza kusaidia malengo ya wafanyabiashra, ili kuweza kujengewea uwelewa katika suala zima la ulipaji wa kodi”alisema.
Aidha Mkuu huyo wa Wilaya alisema, kuanzishwa kwa klabu hiyo itaweza kutoa mwangaza kwa wafanyabiashara, kupata mafunzo mbali mbali ya biashra, pamoja na kuelimishwa juu ya utunzaji wa kumbukumbu za biashara, masoko, huduma nzuri kwa wateja, upangaji wa bei, sheria za biashara na mahesabu ya fedha.
Aidha aliwataka wafanyabiashara kufanya utafiti kwa kina wa biashara wanayotaka kuifanya, kabla ya kuomba mkopo ili fedha wanazopatiwa waweze kuzitumia kwa malengo yaliyokusudiwa, pamoja na benki kufuatilia wafanyabiashara waliowapatia mikopo na kujuwa biashara zao ipasavyo.
Meneja wa NMB kanda ya Dar es Salam Badru Iddi, alisema NMB imeamua kuwafikia wananchi wote wa kipato cha chini Tanzania nzima, kwani mwaka 2018 walifungua klabu za wafanyabiashara 50 Tanzania na mwaka 2019 mikakati yao ni kufungua klabu 36 Tanzania ikiwemo ya Kisiwani Pemba.