WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe, amesema hoja ya Mbunge wa Geita (CCM), Joseph Kasheku Musukuma, kuwa wasanii nchini wanamiliki madanguro na kula fedha za misiba, si ya kweli.
Mwakyembe ametoa kauli hiyo leo Jumanne Aprili 23, 2019 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu hoja za wabunge walizozitoa katika mjadala wa bajeti ya wizara hiyo.
Alhamisi iliyopita Aprili 18, 2019 naibu Spika, Dk Tulia Ackson aliitaka Serikali leo kujibu madai ya wasanii wa filamu nchini kumiliki madanguro sambamba na kuchangisha fedha katika misiba na kuzitumia katika mambo mengine.
Suala la wasanii kumiliki madanguro na kutafuna fedha za misiba liliibuliwa na Musukuma katika mjadala huo na kumfanya Tulia kutaka maelezo ya serikali kwa kuwa kauli hiyo ikiachwa hivyo inaweza kuleta picha mbaya kwa wasanii.
Katika majibu yake Mwakyembe amesema: “Vitendo hivyo havikubaliki kisheria na ni kosa la jinai, nimuombe tu Waziri wa Mambo ya Ndani asilichukulie kwa nguvu suala hili (la madanguro na fedha za misiba) maana Musukuma alizungumza tu pengine kutaka kusikika tu.”
Katika maelezo yake ya Alhamisi iliyopita Tulia alisema:“Kuna mchango ulitoka hapa naamini utakapopewa fursa ya kuhitimisha hoja yako utaliweka vizuri zaidi. Umekuja mchango kuhusu wasanii kuwa ndiyo wamiliki wa madanguro mengi Dar es Salaam.
“Nadhani hili uliweke sawa halitakuwa jambo jema kama halina ukweli wowote kuwadhalilisha wasanii wetu,” alisema Tulia akimtaka pia Mwakyembe kulielezea suala la fedha za mazishi.