
TELEVISHENI bora ya mtandaoni, Global TV Online imezindua rasmi Kipindi cha Global Jamii, ambacho ni maalum kwa ajili ya kuwamulika watu mbalimbali wenye mtatizo ya kiafya, kijamii na wenye kuhitaji msaada kutokana na matatizo yanayowazunguka katika jamii wanayoishi.

Hafla ya uzinduzi huo imefanyika leo, Jumatatu katika ofisi za Global Group zilizopo Sinza Mori jijini Dar es Salaam ikiongozwa na Mhariri Mtendaji wa Global Publishers, Saleh Ally ‘Jembe’ na kuhudhuriwa na Mkurugenzi wa Mtendaji wa Global Group, Eric Shigongo, Meneja Mkuu, Abdallah Mrisho, wafanyakazi.

Pia hafla hiyo imehudhuriwa na mgeni mwalikwa, Mohammed Bane ambaye aliwahi kufanyiwa mahojiano na Global Jamii baada ya kunusurika kifo kufuatia kugongwa na treni wakati akitoka shule na mikono yote miwili na mguu mmoja kukatika.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Shigongo amesema: “Nawapongeza sana timu yote ya Global Jamii na wafanyakazi wote kwa kazi nzuri wanayoifanya.

“Nafahamu ugumu wa kufanya kazi hii kwa sababu hata mimi niliwahi kufanya miaka 20 iliyopita wakati naanzisha kampuni Global Publishers, nilikuwa nikienda hadi vijijini kuhoji watu mbalimbali wenye matatizo makubwa, hivyo napenda kuwatia moyo endeleeni kuongeza bidii.

“Kusema kweli kipindi hiki kinagusa maisha ya watu moja kwa moja na kinawasaidia watu wengi kupitia nyinyi. Wapo waliokuwa hawana fedha za matibabu lakini kupitia kipindi cha Global Jamii wameweza kuonwa na wasamaria wema, mashirika na taasisi mbalimbali.

“Wapo ambao wamewasaidiwa kupelekwa hata India kwa ajili ya matibabu, na kunusuru maisha yao, kwa hiyo msichoke kazi hii ni kama utume, endeleeni kuisaidia jamii, sisi tutaendelea kuwasapoti kwa nguvu zote,” alisema Shigongo.

Aidha, Shigongo alitumia nafasi hiyo kumtia moyo kijana Mohammed ambaye kwa sasa yupo kidato cha nne na kumtaka kutokata tamaa kwani ipo sababu kubwa ya Mungu kumbakisha mzima baada ya ajali ya kugongwa na treni, huku akimuahidi kuwa Kampuni ya Global Group itagharamia masomo yake ya kidato cha tano na sita.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Global Group, Abdallah Mrisho amewapongeza waandaaji wa kipindi hicho na kuwataka wafanyakazi wengine wa Global TV Online kuendelea kuwapa ushirikiano na kuongeza ubunifu zaidi katika vipindi vingine vinavyorushwa kwenye televisheni hiyo.

Naye Mhariri Mtendaji, Saleh Ally amesema; “Napenda kuwaambia nyinyi mnaoendesha kipindi hiki, Anna na Kamonga, uzinduzi wa kipindi hiki uwe chachu ya kufanya kazi bora zaidi, sisi tunaamini ninyi ni bora na mnaweza kukifanya kipindi hiki kiikuze Global na kuwakuza na nyinyi wenyewe.

“Desturi ya Global miaka yote ni kufanya kazi kwa ukaribu na jamii inayotuzunguka, tumejitoa kuisaidia jamii na kupitia kipindi cha Global Jamii, tunaamini watu wengi watatatuliwa matatizo yao na kupata misaada ili waweze kuzifikia ndoto zao, “ alisema Saleh.

Kwa upande waendeshaji wa kipindi hicho, Anna na Kamonga kwa pamoja walitoa shukrani kwa uongozi na wafanyakazi wote wa Global Group, kwa ushirikiano wanaowapa katika kufanikisha kazi yao, huku wakiahidi kujituma zaidi licha ya changamoto mbalimbali wanazokutana nazo wakiwa wanafanya kipindi hicho.

Sambamba na hilo timu ya Global Jamii, ilitoa vifaa mbalimbali vya shule vikiwemo madaftari, viatu, sare za shule, tranka, traki suti na vifaa vingine ambavyo vitamsaidia katika masomo yake.

Kipindi cha Global Jamii huruka kupitia GLOBAL TV ONLINE


HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS/ GPL