



BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imewahamasisha watanzania kutumia akaunti ya malengo ya benki hiyo kama suluhisho ya changamoto mbalimbali za kifedha hivyo kuwawezesha kutimiza malengo ya ndoto zao.
Akizungumza jijini Dar es Salaam leo kwenye droo ya tatu ya kampeni ya Ibuka kidedea na NBC Malengo, Meneja Chapa na Mawasiliano wa benki hiyo, David Raymond alisema kwamba wateja wa benki hiyo waendelee kutumia benki hiyo ili kutatua changamoto zao za kila siku.
“Huu ni mwanzo wa mwaka na watanzania wengi wanakabiliwa na majukumu kadhaa kama vile ada za shule, kodi za nyumba na bima za gari na nyumba, ni muhimu kwao kuendelea kuwa karibu na benki hii na kwa wale ambao bado hawajafungua akaunti ya malengo ni vyema wakufungua ili waweze kunufaika na zawadi,” alisema Raymond.
Meneja huyo wa Chapa na Mawasiliano alisema kwamba droo hiyo ni ya tatu ambayo ilianza mwezi wa Oktoba mwaka jana na washindi kadhaa wa bodaboda na safari za kutalii mbuga za wanyama Serengeti na Visiwani shelisheli walikwenda na kurudi salama kwa usimamizi na ufadhili wa benki hiyo kupitia kampeni ya malengo akaunti.
Kwenye droo hiyo ya jana washindi watano waliibuka kidedea kwa kujishindia pikipiki aina ya Yamaha, washindi hao ni; Luka Haule Baraka wa Dodoma, Juma Halfani kutoka Songea, Rebeka Ndosh anayeishi Mwanza, Rosemary Kibodya wa Dar es Salaam na Restituta Mbuya wa Morogoro.
Kampeni ya Ibuka Kidedea na NBC Malengo itashuhudia washindi watatu wakiibuka kidedea na kujishindia zawadi ya pikipiki ya miguu mitatu aina ya Toyo katika droo kubwa inayotarajiwa kufanyika Mwezi Machi mwaka huu.