×

CSI Yatoa Msaada kwa Kaya Zaidi ya 50 Wasiojiweza Ukonga

Shirika la kimataifa la Childbirth Survival International (CSI), limetoa msaada wa vyakula , sukari na sabuni kwa kaya zaidi ya 50 za watu wasiojiweza zinazoishi Kata ya Mazizini Ukonga jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa CSI ni kwamba kutokana na uwepo wa virusi vya Corona nchi nyingi barani Afrika ikiwemo Tanzania wananchi wanapita kwenye wakati mgumu, hivyo kwa kutambua hilo wameamua kutoa msaada huo kwa jamii ya watanzania na hasa yenye uhitaji.

 

Akizungumza Mei 2, 2020 jijini Dar es Salaam wakati wa utoaji wa msaada huo, Mkurugenzi wa CSI nchini Tanzania Stella Mpanda amesema wamekuwa wakihusika kusaidia wanawake,wajawazito na vijana lakini kwa wakati huu wa Corora kupitia ofisi zao zilizoko Marekani na za hapa nchini Tanzania wameamua kuwakarimu wanananchi wasiojiweza wa kata ya Mazizini.

 

“Wananchi hawa ambao hawana uwezo wamekuwa wakipata changamoto kwenye utafutaji riziki na kipindi hiki cha Corona hali zao kiuchumi ni mbaya zaidi, hivyo shirika letu limeamua kuwasaidia vyakula vya aina mbalimbali, sukari na sabuni.

“Kwa hiyo tumeona tuwasaidie kwa kiasi, kwa kuchukua hiki kidogo ambacho tunacho, kwa siku ya leo tumesaidia zaidi ya kaya 50 na wote hao tumewapa mchele, sukari maharage,unga na mche wa sabuni,hivyo ambavyo tumetoa kwetu tunaona ndio jambo la msingi. Tutaendelea kusaidia jamii yenye uhitaji kadri tutalavyojaaliwa kupitia wadau wetu mbalimbali”amesema Mpanda.

 

Kuhusu Corona, Mpanda amesema pamoja na kutoa msaada huo, wametumia nafasi hiyo kuwahamasisha wananchi kuendelea kuchukua tahadhari zinatolewa na Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ili kukabiliana na ugonjwa huo hatari.

Mpanda amesema kuwa kasi ya maambukizi ya Corona kwa sasa ni kubwa, hivyo ni muhimu wananchi kuendelea kuvaa barakoa, kunawa maji tiririka na sababu , kupaka vitakasa mikono huku akisisitiza ugonjwa huo ni halisia na unaua.

 

“Kwa hali ilivyo ni lazima tuchukue tahadhari na kubwa zaidi tujitahidi kuepuka mikusanyiko ambayo haina ulazima na ni bora kwa wale ambao hawana sababu ya kutoka nje ya nyumba zao wakabaki nyumbani tu, hii itasaidia kupunguza kasi ya maambukizi,” amesema Mpanda.

 

 

 

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Kata ya Mazizini Ukonga jijini Dar es Salaam Mussa Komba ametoa shukrani kwa niaba ya wananchi kutokana na msaada huo huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kufuata maelekezo ambayo yanatolewa na Wizara ya Afya na ili kukabliana na ugonjwa huo kila mtu kwa nafasi yake anatakiwa kuchukua hatua ikiwemo ya kufuata maelekezo ya watalaam wa afya.

Mmoja ya wananchi aliyepata msaada huo Habiba Tawaqal amesema anashukuru CSI kutoa msaada huo ambao umewafariji na kubwa zaidi umekuja wakati mauafaka na kuhusu Corona ni vema jamii kutambua umuhimu wa kuvaa barakoa kwani ugonjwa huo ni hatari.

Leave a Comment