
RAIS John Magufuli ameeleza nia yake ya kufungua shule za Awali, Msingi na Sekondari baada ya kuona hali ya ugonjwa wa Corona inavyoendelea kupungua.
Akizungumza leo katika Mkutano Mkuu wa Chama Cha Walimu Tanzania unaofanyika katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma, amesema serikali ipo mbioni kufungua shule kwani anajua walimu wa Tanzania wanapenda kufanya kazi.
Amesema taarifa alizopata juzi kutoka kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, kuwa mpaka juzi kulikuwa na wagonjwa wanne kutoka Dar es Salaam, hivyo hali ya ugonjwa inapungua.
“Walisema kwa Afrika maiti zitazagaa ila Mungu wetu anatupenda, taifa hili tuliomba maombi siku tatu na juzi Dar es Sala niliambia kuna wagonjwa wanne …uzushi utatolewa wa kila aina ila leo naona walimu hapa hamjavaa barakoa,” amesema na kuongeza:
“Nashukuru Mungu na Watanzania, tumeshinda na tukaendelee kushinda, nina hakika hivi karibuni baada ya kufungua vyuo, tunaangalia mambo yanavyoenda na shule za msingi na chekechea nazo ziko mbioni tutazifungua ili walimu wakafanye kazi,
“Hapa leo tunaonana nilikuwa namuangalia Spika akiwa anaongoza Bunge yupo pekee yake kwenye kiti chake lakini kavaa barakoa…tumtangulize Mungu katika hili,” amesema.
Aidha amesema mtu yeyote atakayempa mtu barakoa akatae ni bora mtu kuamua kushona mwenyewe lakini sio kuchukua barakoa isiyojulikana imetoka wapi. Watanzania tutaumia kwa kukosa maarifa hivyo mtu akitaka kuvaa barakoa ni vyema ashone yake mwenyewe, amsema.
“Tupo Watanzania millioni sitini kila mmoja achukue tahadhari hivyo kwa kupokea barakoa na hujui imetoka wapi ni hatari …ugonjwa huu umepungua tumeanza na Mungu tutamaliza na Mungu,” amesema.