MGOMBEA urais kwa tiketi ya Chama cha Union for Multiparty Democracy (UMD), Mohamed Mazrui, amesema iwapo atapata ridhaa ya kuongoza Tanzania, serikali yake itafuta utaratibu wa wananchi kupewa vitambulisho vya taifa.
Alisema hayo juzi wakati wa mkutano wa kampeni uliofanyika Mbagala, jijini Dar es Salaam alipobainisha kwamba baada ya kufuta utaratibu wa kutoa vitambulisho hivyo, wananchi watapewa hati za kusafiria (passport) ambazo zitatolewa bure nchi nzima.
Alisema, hati hizo zitawawezesha wananchi hao kusafiri katika nchi yoyote kwa ajili ya kwenda kutafuta maisha, bila vikwazo vyovyote. Kuhusu ajira, alisema serikali yake itapunguza masharti kwa wawekezaji, ili waweze kuwekeza kwa wingi na hivyo kuongeza ajira kwa wananchi.
Alifafanua kwamba wakulima watanufaika kwa kutafutiwa wanunuzi wa kimataifa ambao watanunua mazao kwa bei nzuri.
“Wakulima tutawaondolea suala la stakabadhi ghalani badala yake tutawaletea wanunuzi wa mazao kutoka nje,” alisema. Aliongeza kuwa, serikali yake itaondoa utaratibu wa kulipa kodi ya majengo, ambayo imekuwa kero kwa wananchi.
Vilevile, alisema hivi sasa wananchi wanatozwa kodi ya majengo, lakini katika hali ya kushangaza huduma kama za taka wanatozwa tena fedha, jambo ambalo linaleta usumbufu. Aliongeza pia kuwa walimu wataongezewa mishahara na elimu itaboreshwa na kuwa bure japo wananchi watachangia kiasi kidogo.
