MSHAMBULIAJI mpya wa Simba, Chris Mugalu amesema kuwa amefurahi kuona anafunga katika mchezo wake wa kwanza wa ligi kuu huku akimsifia Chama kutokana na pasi aliyompa iliyosababisha yeye kufunga bao.
Mugalu alisajiliwa na Simba akitokea Lusaka Dynamo ya Zambia, ambapo katika mchezo wake wa kwanza wa ligi aliifungia Simba bao la nne katika ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Biashara, mchezo uliochezwa katika Uwanja wa Mkapa jijini Dar.
Akizungumza na Championi Jumatano, Mugalu alisema kuwa anafurahi kuona amefunga bao katika mchezo wake wa kwanza wa ligi kuu ambapo anaamini kufanya hivyo kutampa hali ya kujiamini kwa kufanya vizuri katika michezo inayofuata ya ligi huku akimpongeza Chama kwa kumpatia pasi nzuri ambayo hakuitegemea.
“Nimefurahi kufunga katika mchezo wangu wa kwanza wa ligi hii itaniongezea kujiamini katika michezo yangu inayofuata kucheza kwa kujiamini, ukiwa kama mshambuliaji lazima udaiwe mabao hivyo kama hautafunga basi utacheza kwa wasiwasi lakini kwangu nashukuru nimefunga.
“Kuhusu pasi ya Chama nimefurahi kuona kanipa pasi nzuri,nilikuwa nimekaa sehemu nzuri ya kufunga lakini sikutarajia kama Chama angenipigia pasi kama ile,ila nashukuru kwa kuwa alinipa na nikafunga,”alisema mchezaji huyo.
Mugalu tangu atue Simba amefanikiwa kutumikia michezo miwili dhidi ya Vital ‘O na Biashara ambapo katika michezo hiyo alifanikiwa kufunga mabao mawili huku akifunga katika kila mchezo.
Stori: Marco Mzumbe, Dar es Salaam

