
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa usiku wa kuamkia leo Januari 30, 2021, amemtangaza Yusuph Nizar kuwa Mshindi wa BSS kwa msimu huu wa 11 kwa mwaka 2021 katika Ukumbi wa Ubungo Plaza jijini Dar es Salaam.
Nizar aamefanikiwa kuibuka mshindi wa kitita cha sh. milioni 20, katika shindano la Bongo Star Search (BSS) ‘Kubwa na Nusu’ huku akiwapoteza wenzake sita aliotinga nao katika hatua ya fainali hizo.

Mbali na Yusuph kuibuka mshindi, shindano la mwisho kufanyika lilikuwa ni mwaka jana ambapo Meshack Fukuta, aliibuka kidedea na kujizolea kitita kama hicho cha sh. milioni 20, japo baadaye alisikika akilalamika kutopewa pesa hizo.

Katika shindano hilo, mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa, ambaye alimkabidhi mshindi huyo mfano wa hundi ya shilingi milioni 20.

Katika hafla hiyo, Bashungwa alisema: “Nitumie wasaa huu, kuwapongeza waandaaji wa shindano hili, hususani Madam Rita na wadhamini wote waliojitokeza kusapoti mashindano haya, sina shaka kwamba kila Mtanzania mwenye kupenda sanaa atahakikisha anaendeleza vipaji hivi ili viweze kutanua wigo wa ajira hapa nchini,” alisema.