
KUNDI linalojiita Dola la Kiislamu, IS limedai kuhusika na shambulizi la bomu lililoua Mtu mmoja kwenye Mji Mkuu wa Uganda, Kampala Jumamosi usiku, haya yameelezwa kupitia ukurasa wa Telegram wenye mafungamano na kundi hilo ambapo IS imesema wamelipua bomu hilo katika Club moja ambayo Majasusi wa Serikali ya Uganda hupendelea kukaa.
Taarifa ya polisi wa Uganda imesema kuwa shambulio hilo liliilenga baa inayouza nyama ya nguruwe katika kitongoji kimoja cha Mji wa Kampala ambapo Wanaume watatu waliingia kama Wateja wakaweka mfuko wa plastiki wenye vilipuzi chini ya meza na kisha wakaondoka kabla ya mlipuko.
Rais wa Uganda Yoweri Museveni amesema shambulio hilo linaonekana kuwa la kigaidi, mbali na mmoja aliyeuawa, shambulio hilo liliwajeruhi wengine watatu, wawili wakiwa katika hali mahtuti ambapo baada ya IS kukiri kuhusika na mlipuko huo wameiita Serikali ya Uganda kama Adui wa Uislamu.