
SERIKALI imesema watoto 157 wamefariki huku idadi ya washukiwa nchini kote ikiongezeka maradufu katika muda wa siku nne.
Wote waliokufa hawakuwa wamechanjwa dhidi ya surua kulingana na maafisa wa afya.
Jumla ya kesi zinazoshukiwa kote nchini zimeongezeka kutoka 1,036 hadi 2,056 katika muda wa siku nne pekee, Waziri wa Habari Monica Mutsvangwa alisema Wizara ya Afya hapo awali ililaumu mikusanyiko ya madhehebu ya kidini kusababisha kuzuka kwa ugonjwa huo.

Maambukizi ya kwanza yaliripotiwa mapema mwezi huu, kesi nyingi zilizoripotiwa huhusisha watoto wenye umri wa kati ya miezi sita na miaka 15 kutoka madhehebu ya kidini ambao hawaamini katika chanjo.
“Imebainika kuwa kesi nyingi hazijapata chanjo ya kujikinga na surua. Serikali imetumia Sheria ya Kitengo cha Ulinzi wa Raia kushughulikia dharura hii.” alisema Mutsvangwa.
Pia alisema serikali itaongeza chanjo na akataja sheria maalum inayoiruhusu kupata pesa kutoka kwa hazina ya kitaifa ya maafa “ili kukabiliana na janga hilo.”

Mwezi Aprili, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilisema Afrika inakabiliwa na mlipuko wa magonjwa yanayoweza kuzuilika kutokana na ucheleweshaji wa utoaji chanjo kwa watoto, huku wagonjwa wa surua wakiongezeka kwa asilimia 400.
Imeandikwa:Dunstan Mtili Erick Kwa msaada wa mitandao