
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akishuhudia tukio la kuanza kujaza maji Kwenye Bwawa la kufua umeme la Julius Nyerere (JNHPP) lililopo Rufiji, Mkoani Pwani leo tarehe 22 Desemba, 2022
Rais Samia amefunga geti hilo leo Desemba 22, 2022 kabla ya kutoa hotuba yake katika hafla ya kuanza kujaza maji kwenye bwawa hilo lililopo Rufiji, Mkoani Pwani.

Awali Waziri wa Nishati, Januari Makamba amesema ili tuta lijengwe ni lazima sehemu hiyo iwe kavu pasiwe na mto unapita hivyo walijenga handaki la kuchepusha mto ili kufanikisha ujenzi huo.
“Handaki lilikamilika mwaka 2019, mto Rufiji ukawa unapita kwenye hilo handaki na ujenzi wa tuta ukaanza na leo tumefika hatua ya kukamilika kwa tuta hili kwa kiwango cha kuweza kujaza maji na kwa kuwa kuna mvua tukaona ni wakati muafaka kwa maisha ya mradi tuzibe lile handaki ili mto huu urudi kwenye njia yake,” amesema Makamba.

Amesema maji kwa kiwango kilichotathminiwa kimazingira yataendelea kupita na kuwanufaisha wakazi wa maeneo jirani hivyo wananchi waondoe taharuki.
“Tunaziba handaki ambalo litawezesha mto Rufiji urudi kwenye njia yake ya asili handaki hili lenye mita 19 tumetengeneza geti tutakaloziba leo lenye uzito wa tani 368 na baada ya kufungwa kwa geti hili itachukua muda wa kama dakika 30 maji yataanza kujaa hapa,” amesema Waziri Makamba.