
KATIKA kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini, Kampuni ya Oryx Gas kwa kushirikiana na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kilimanjaro Shally Raymond wamegawa bure mitungi ya gesi 1000 yakiwa na majiko yake kwa viongozi wa dini na wajasirliamali wa mkoa huo.
Lengo la kugawa mitungi kwa vingozi wa dini ni kutambua mchango wao kwa jamii hasa kwa kuzingatia ni kundi ambalo likipata elimu ya kutosha kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira kwa kutumia nishati safi ya kupikia, watakuwa mabalozi wazuri na kuhamasisha matumizi ya nishati hiyo kama sehemu ya kulinda mazingira kwa kuacha kutumia kuni na mkaa.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukagwa mitungi hiyo kwa viongozi wa dini na wajasriamali wa mkoa huo, Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga ametumia nafasi hiyo kuwaomba viongozi wa dini kutumia nafasi zao kujikita pia katika kusaidia jamii kutambua umuhimu wa kutunza mazingira kwa kuachana kutumia kuni na mkaa.
“Viongozi wa dini ni watu wa thamani sana , unajua sisi binadamu watu ambao tunawathamini na kuwasikiliza ni viongozi wetu wa dini na mimi kwa utashi wangu mdogo naamini tunawasikiliza viongozi wa dini kwasababu kazi ya kueneza neno la Mungu hakuna anayelipwa.Kwa maana hiyo ndio maana mama Shally pamoja na makundi mengine yote ameamua kuleta viongozi wa dini kwani sisi tunawaheshimu tuna matumaini makubwa na viongozi wa dini.Tunaamini viongozi wa dini wanaweza kusaidia kuwaelimisha jamii kutunza mazingira,”amesema Naibu Waziri Kapinga.
Pia amesema uharibifu wa mazingira unatokana na ukataji miti imessababisha hata mikoa iliyokuwa na mvua nyingi kama mikoa ya nyanda za juu kusini ambazo zilitakiwa mvua kuanza Novemba zinaanza mwishoni mwa Desemba.Hiyo inatokana na matendo yetu wenyewe ya kuharibu mazingira.

“Tunaamini viongozi wa dini mpo katika nafasi ya kutusaidia kuendelea kukumbusha jamii kwamba dunia hii ambayo tumepewa zawadi na Mwenyezi Mungu ni haki ya kila mmoja kuilinda leo, tunawatoto na wajukuu na tutakuwa na vitukuu pia, sasa kama rasilimali zote zilizopo zikachezewa wajuu na vitukuu wataishi katika mazingira gani?”
Pia amesema kuwa katika kampeni hiyo ya kuhamasisha matumizi ya nishati ya kupikia wamekuwa wakihusisha zaidi wanwake kwasababu wanawake ndio wanaokaa jikoni kupika kuandaa chakula.“Kwahiyo mwaka 2024 tusikubali kupika kwa kuni wala mkaa.

“Tunawashukuru Oryx kwa kutupatia majiko ya gesi lakini njia za nishati safi ya kupikia ni ile tu kasumba kwamba hii ni gharama lakini ndugu zangu kibaba cha mkaa wa Sh.2000 jioni hakifiki.Ni gharama nafuu kutumia nishati safi kuliko kutumia kuni na mkaa katika kuandaa chakula.”
.Akizungumzia kampeni ya nishati safi ya kupikia, Naibu Waziri Kapinga amesema mwaka jana mwishoni kulikuwa kuna mkutano wa dunia wa mazingira na katika mkutano huo Rais Dk.Samia Suluhu Hassan alienda na ajenda mahususi ya kumkomboa mwanamke wa Afrika sio mwanamke wa Tanzania peke yake.
“Kumkomboa vipi?Kuweka mikakati ya kuhakikisha wanawake wote wa Afrika wanatumia nishati safi ya kupikia na katika mkutano ule ulihusisha wakuu wa nchii. Rais Dk.Samia kutokana na umahiri wake na uwezo wake aliweza kukusanya viongozi na kuzindua program maalum kusaidia wanawake wa Afrika kwenye kutumia nishati safi ya kupikia.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Oryx Benoite Araman, Meneja Mauzo wa Kampuni hiyo Shaban Fundi ameeleza kwamba wanajivunia kuwezesha makundi mbalimbali yakiwemo wanawake, watoto na wajasiriamali kupata nishati safi ya kupikia.

Amefafanua kuwa kufanya hivyo wanaamini wanaikomboa jamii na taifa kwa ujumla wake kwani kupika kwa gesi ya Oryx kuna maanisha kuboresha afya za kinamama kwa kueuka kuvuta moshi mbaya wa kuni na mkaa.Pia watoto watapata muda wa kwenda shule badala ya kutumwa kutafuta kuni.
Amesisiza kampuni hiyo kwa kutambua nafasi ya viongozi wa dini imeona ni vema sasa ikatoa mitungi ya gesi ya Oryx na majiko yake kwa kundi hilo sambamba na kuelezea kwa kina umuhimu wa kutunza mazingira na wanaamini kuwa viongozi wa dini wana nafasi kubwa ya kusema na kusikilizwa, hivyo watakapokuwa mabalozi wa kuzungumzia nishati safi ya kupikia jamii itabadilika na hivyo kuokoa mazingira.
Aidha amekumbusha kuwa mwaka 2021 Rais Dk.Samia Suluhu Hassan alianzisha kampeni ya nishati safi ya kupikia na alitoa maono yake ya kwamba ifikapo mwaka 2032 asilimia 80 ya wananchi itumie nishati safi, hivyo kuanzia hapo Oryx iliongeza nguvu na hadi sasa ya mitungi 19000 bure yenye thamani isiyopungua Sh.bilioni 1.5.