
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Dr. Charles E. Msonde amekutana na walimu wote wa Shule za Msingi, Sekondari, Walimu Wakuu, Wakuu wa Shule, Maafisa Elimu Kata, Wadhibiti Ubora wa Shule, Maafisa Elimu wa Msingi na Sekondari, Maafisa wa Tume ya Walimu (TSC) na viongozi wengine kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Karatu wakiongozwa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Mwl Yusuph Hamza
NKM OR-TAMISEMI amezungumza na Walimu na kueleza changamoto Kuu 6 zinazowakumba walimu ikiwa ni pamoja na kupandishwa Madaraja, kubadilishwa Muundo, Mshahara wa daraja jipya kuchelewa kubadilishwa na malimbikizo ya mishahara kuchukua muda mrefu kulipwa( Salary Arreas), fedha za Uhamisho hazitoki kwa wakati, fedha za likizo pamoja na kuthaminiwa pale wanapowasilisha changamoto zao kwa viongozi.

Sambamba na hayo, NKM OR-TAMISEMI ameelekeza Maafisa Elimu Msingi na Sekondari kuhakikisha wanachukua taarifa zote za walimu wanaodai madai yao na kuziwasilisha wenyewe kwa Maafisa utumishi ili wazifanyie kazi na kuondokana na changamoto za madai ya walimu hao.
Aidha NKM, amesisitiza utumike utaratibu wa wakwanza awe wa kwanza ili haki itengeke katika kulipa madeni ya walimu.
” Madeni yasiwe siri, orodha iwekwe wazi na walimu walipwe kulingana na orodha wa kwanza awe wa kwanza na wa mwisho awe wa mwisho. Tusilipe kwa upendeleo.” amesema Dr. Msonde.

Pia, NKM, amesisitiza kuitambua hadhi ya walimu kwani ndio wanaozalisha madaktari, wahandisi, marubani na taaluma nyingine, hivyo walimu waheshimiwe kama taaluma nyingine.
Mwisho amewataka walimu kufundisha kwa Maarifa, bidii, na kuwa wabunifu, katika ufundishaji na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kuboresha taaluma kwa wanafunzi na kufikia dhamira ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Rais Dr. Samia Suluhu Hassan Katika maboresho chanya kwenye Sekta ya Elimu nchini.