
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imetoa ufafanuzi kuhusu taarifa zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu kuvunjwa kwa nyumba iliyokuwa imejengwa kwenye Kiwanja Na. 318 Kitalu ‘J’
Mbezi, Manispaa ya Kinondoni.
Taarifa hizo zinaeleza aliyetekeleza zoezi la kuvunja anatajwa kuwa ni Bi. Jacqueline Noni huku kumbukumbu zilizopo zikionesha kiwanja hicho kilimilikishwa awali kwa Hati Milki iliyosajiliwa kwa Na. 29350 mwaka 1983 kwa muda wa miaka 33 kwa Ndugu Costa James Ninga wa S. L. P 2108, Dar es Salaam.
Taarifa ya ufafanuzi ya Wizara inabainisha kuwa Mwaka 1993 Ndugu Costa James Ninga alihamisha milki yake kwa njia ya mauziano kwenda kwa Bi Jacqueline
Noni kwa gharama ya shilingi 500,000 na kibali cha uhamisho huo kupata kibali cha
Kamishna wa Ardhi.
“Aidha, baada ya milki yake kuisha, ilihuishwa tena kwa miaka 99
kuanzia mwaka 2015. Kiwanja hiki kimekuwa na mgogoro wa muda mrefu unaohusisha uvamizi uliofanywa na
mlalamikaji na umekuwa ukishughulikiwa kiutawala katika ngazi mbalimbali za mamlaka
ikiwemo ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni na Wizara.”
“Vilevile wakati wa zoezi la
kliniki ya ardhi katika eneo la Bunju lililoendeshwa na Wizara mwezi Februari na Machi
2024 wahusika kwenye mgogoro huu walipata fursa ya kusikilizwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Jerry William Silaa.” —Wizara
Baada ya wahusika kusikilizwa na kupitia taarifa za umiliki, ilibainika kuwa mmiliki halali wa kiwanja tajwa ni Bi. Jacqueline Noni. Aidha, ilielekezwa ili kumaliza mgogoro huu,
wahusika watekeleze yafuatayo
1) Mvamizi akubaliane na mmiliki kumlipa fedha;
2) Mvamizi amtafutie kiwanja kingine mmiliki; na
3) Mvamizi aondoshe jengo lake au avunjiwe kiwanja kiwe huru kwa mmiliki halali.
Maamuzi haya yalizingatia haki ya Bi. Noni ambaye kwa miaka 31 tangu alipomilikishwa ameshindwa kutumia mali yake halali kama Ibara ya 24 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Toleo la Mwaka 1977 inavyotaka badala ya kuangalia nyumba ya mvamizi iliyobomolewa.
