
Viongozi wa dini wametakiwa kuwa mfano na vinara katika kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia hasa kwa watoto katika jamii inayowazunguka ili kuhakikisha havitokei katika maeneo yao.
Wito huo umetolewa na Nabii Nicolaus Suguye wakati alipokuwa katika ziara ya kutembelea vituo viwili vya kulelea watoto yatima vilivyopo mkoani Morogoro ambapo ametembelea vituo mbalimbali kama Raya Islamic Foundation chenye jumla ya watoto 90 na Kituo cha Dar_Ulmuslimeen Orphanage chenye jumla ya watoto 67 na kutoa misaada mbalimbali ya mahitaji kwa watoto wanaoishi katika vituo hivyo.

Nabii Suguye amesema vitendo vya ukatili kwa watoto vinafanywa na watu wa karibu hivyo viongozi wa dini wametakiwa kutumia nyumba za ibada kukemea vitendo hivyo ambayo vimeshika kasi kwa siku za hivi karibuni.
Amesema katika maeneo mengi imezuka tabia ya watoto kuibwa, kuuawa na kukatwa viungo vya mwili, jambo ambapo linahatarisha usalama wa watoto hivyo kila mtu anawajibu wa kupambana na vitendo hivyo.
Aidha, amewataka wazazi kuwa karibu na watoto wao katika malezi badala ya kuwaacha kutembea mitaani na kuiga mambo yasiyokuwa ya utamaduni wa Kiafrika.
Katika ziara hiyo, Nabii Suguye ametoa misaada wa vitu mbalimbali ikiwemo magodoro, mchele, unga, mafuta ya kupikia, madaftari, pamoja na taulo za kike.
Ziara hiyo ya Nabii Suguye ni maandalizi ya mkutano mkubwa wa injili utakaofanyika mkoani Morogoro katika Viwanja vya Sabasaba kuanzia Julai 24 hadi Julai 28, 2024 wenye lengo la kuwafundisha waunini wa dini ya Kikristo kufuata maaandiko matakatifu ya Biblia yenye kumpendeza Mwenyezi Mungu.