
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameungana na Watanzania katika kulaani mauaji ya aliyekuwa kiongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Ali Kibao yaliyosababisha mshtuko na hisia kali nchini.
Akizungumza Septemba 17, 2024, kwenye maadhimisho ya miaka 60 ya Jeshi la Polisi yaliyofanyika katika viwanja vya Chuo cha Polisi Moshi, Rais Samia amesisitiza kwamba mauaji hayo hayakubaliki kwa sababu yoyote ile.

Rais Samia alisema, “Siku kadhaa zilizopita ndugu zangu nchi yetu imepata msiba wa kuuawa kwa mmoja wa viongozi wa CHADEMA, kifo kilichosisimua miili na akili za sisi wananchi na kuibua hisia kali hasa kwa wafuasi wa chama hicho.”
Kifo hicho kimeleta majonzi sio tu kwa Watanzania bali pia kwa wawakilishi wa baadhi ya mataifa ya nje wanaoziwakilisha nchi zao nchini Tanzania.
Rais Samia aliendelea kusema kwamba mauaji hayo hayakubaliki na serikali imechukua hatua za haraka kuhakikisha uchunguzi unafanyika.

“Katika hali ya kushangaza, kifo hicho pia kimeleta hisia kali kwa wawakilishi wa baadhi ya mataifa ya nje wanaowakilisha nchi zao hapa kwetu. Nataka niungane nao niseme kwamba kwa sababu yoyote ile mauaji haya hayakubaliki,” amesema Rais Samia.
Ameongeza kuwa serikali imechukua hatua za haraka kuanzisha uchunguzi juu ya mauaji hayo na kwamba kazi ya uchunguzi inaendelea kwa ufanisi. “Ndiyo maana tuliyalaani na kutaka uchunguzi wa haraka ufanyike na ndivyo inavyofanyika duniani kote na kazi nimeambiwa inaendelea vizuri,” amesema Rais.