
Katika kuenzi uzazi na mchango mkubwa wa wanawake katika jamii, Benki ya I&M imezindua rasmi Chumba Maalum kwaajili ya Wamama eneo tulivu, lenye faraja na lililobuniwa kwa umakini mahsusi kwa ajili ya kuwawezesha na kuwaunga mkono wamama wakiwa katika mazingira yao ya kazi.
Chumba hicho, kilichopo katika makao makuu ya benki hiyo, kimetengwa kwa ajili ya wamama wanaonyonyesha na wanaofanya kazi, kikiwa na mazingira ya faragha, usafi wa hali ya juu na utulivu—mahali salama pa kunyonyesha, au hata kupumzika kwa muda. Hatua hii inaonyesha kwa vitendo dhamira ya Benki ya I&M katika kujenga mahali pa kazi jumuishi, rafiki kwa familia na wenye kuzingatia mahitaji ya wafanyakazi.
“Chumba hiki si tu huduma ya msingi—ni alama ya heshima, upendo na kuthamini mchango wa wamama. Wamama wanaofanya kazi hukabiliana na jukumu la kazi na kulea, yaani kufanikisha majukumu ya kazi huku wakilea familia zao,” amesema Erica Mboya, Mkuu wa Rasilimali Watu wa Benki ya I&M.

Uzinduzi wa chumba hiki umefanyika wiki ya maadhimisho ya Siku ya Mama Duniani, ikiwa ni sehemu ya juhudi za benki kuunda mazingira yenye huruma na huduma jumuishi kwa wafanyakazi. Hatua hii inaakisi falsafa ya benki kwamba kuwajali watu ni zaidi ya maendeleo ya kifedha, inahusu pia ustawi wa familia zinazowazunguka.
Ndeshi Rajabu, mama na mfanyakazi wa Benki ya I&M, ameeleza kwa furaha:
“Kama mama mpya, kurejea kazini kulikumbwa na changamoto mbalimbali—hasa kutafuta sehemu salama na ya faragha ya kunyonyesha au kupumzika. Chumba hiki kimeleta tofauti kubwa sana. Kinaonyesha kuwa benki inatutambua si tu kama wataalamu, bali pia kama wazazi wenye majukumu halisi ya maisha.”

Kupitia hatua hii, Benki ya I&M inaungana na taasisi za kisasa zinazotambua na kuthamini uzazi kwa vitendo, kwa njia za kuwawezesha wanawake na kuleta mabadiliko chanya kazini. Hii inaashiria kwamba hata hatua ndogo lakini zenye maana zinaweza kuleta mabadiliko makubwa katika maisha ya wafanyakazi.