×

Wakili wa Zamani wa Jeshi la Israel Akamatwa baada ya kuvuja kwa Video ya Unyanyasaji

Tel Aviv, Israel — Wakili wa zamani wa kijeshi wa Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF), Meja Jenerali Yifat Tomer-Yerushalmi, amekamatwa kufuatia sakata la kisiasa lililozuka baada ya kuvuja kwa video inayoonyesha madai ya unyanyasaji mkali dhidi ya mfungwa wa Kipalestina.

Tomer-Yerushalmi, ambaye alijiuzulu wiki iliyopita kama Wakili Mkuu wa Kijeshi wa IDF, alitangaza kuwa anawajibika kikamilifu kwa uvujaji wa video hiyo. Tukio hilo lilichukua sura mpya Jumapili baada ya kuripotiwa kutoweka, na kupelekea polisi kuendesha msako wa dharura kwenye fukwe za kaskazini mwa Tel Aviv. Baadaye alikutwa akiwa hai na mzima, ingawa aliwekwa chini ya ulinzi wa polisi.

Video hiyo, iliyotangazwa kwa mara ya kwanza Agosti 2024 na kituo cha habari cha Israeli, inaonyesha askari wa akiba katika kituo cha kijeshi cha Sde Teiman, kusini mwa Israel, wakimshambulia mfungwa wa Kipalestina. Inadaiwa kuwa askari hao walimzunguka kwa ngao za kutuliza ghasia ili kuficha kitendo hicho, kisha wakampiga na kumdunga na kitu chenye ncha kali sehemu za siri. Mfungwa huyo alilazwa hospitalini kutokana na majeraha makubwa.

Askari watano wa akiba wamefunguliwa mashtaka ya unyanyasaji wa hali ya juu na kusababisha madhara makubwa ya mwili, ingawa wote wamekana mashtaka hayo na hawajatajwa majina. Wanne kati yao walionekana Jumapili wakiwa wamevaa mavazi meusi kuficha nyuso zao walipofika mbele ya Mahakama ya Juu mjini Jerusalem, wakiwa na mawakili wao waliotaka kesi hiyo ifutwe.

Wakili wao, Adi Keidar kutoka shirika la mrengo wa kulia la Honenu, alidai kuwa “wateja wake wanakabiliwa na mchakato wa kisheria uliojaa upendeleo na usio wa haki.”

Video hiyo imeibua mjadala mkubwa nchini humo, huku upande wa kushoto ukitaja kama ushahidi wa wazi wa ripoti za muda mrefu kuhusu unyanyasaji wa wafungwa wa Kipalestina tangu shambulio la Hamas la Oktoba 7, 2023.

Ripoti ya Tume ya Uchunguzi ya Umoja wa Mataifa iliyotolewa Oktoba mwaka jana ilidai kuwa maelfu ya wafungwa kutoka Gaza, wakiwemo watoto, wamekumbwa na “unyanyasaji mkubwa wa kimwili, kisaikolojia, na wa kijinsia unaoweza kufikia kiwango cha uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu.”

Hata hivyo, Serikali ya Israel imekanusha vikali tuhuma hizo, ikisisitiza kuwa imejitolea kufuata viwango vya kimataifa vya haki za binadamu na kwamba kila malalamiko yamechunguzwa kwa kina.

Leave a Comment