The House of Social Media
gunners X

Mkutano Wa Wazee Kuimarisha Haki Umoja Na Amani Kwa Watanzania Yatoka Na Maadhimio Haya

0

Wito umetolewa  kwa Watanzania Kuwajibika na kuwawajibisha wasiowajibika kwa mujibu wa Katiba, Sheria na Kanuni ziongozazo.ili Kuweka maslahi ya Taifa juu ya Ubinafsi, Vyama wala Makundi yoyote. Kushirikiana kwa umoja katika kutatua changamoto na migogoro kwa amani.

Akitoa Maazimio hayo Kwa niaba ya wazee wakati wa mkutano wa wazee wa kuimarisha Haki, Umoja na Amani kwa Watanzania ambao umefanyika Leo, Januari, 22,2026 Jijini Dar-es-Salaam
Mratibu wa Programu wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF) Dk Musuto Chirangi pole kwa Watanzania wote, hususan waliofikwa na madhira yaliyotokana na uvunjifu wa amani uliosababisha vifo na uharibifu wa mali, siku ya na baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2025. Hali hiyo  ilitokea katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu na kwamba hadi sasa tunasubiri taarifa kamili ya usuli wa vurugu na ghasia na pia  madhara halisi kwa uhai,  mali na miundombinu ya umma na binafsi.
Amesema Pamoja na hayo, matukio ya ama Watu kutekwa, kupotea au kuuwawa nayo yameacha hofu kubwa kwa Wananchi na yameathiri misingi ya amani, umoja na mshikamano wa Taifa letu. Yameathiri jitihada za Wananchi kutumia fursa za kiuchumi na ajira kwa maendeleo yao na  nchi yao. Hivi sasa kuna chembechembe za migawanyiko na kushutumiana hususani katika mikabala kidini na kisiasa, jambo lisilo na afya katika ustawi na maendeleo ya nchi.
” Kuhusu Maafa na Uharibifu
Sisi Wazee tunatambua kuwa wote tuko katika maombolezo  ya misiba ya kuondolewa  uhai wa wapendwa wetu, Pasipo kuwa na taarifa kamili, ni busara tuendelee kuwa watulivu na wenye subira. Tulisikitishwa, tunaomboleza na tunazifariji familia zote husika.
“Tunapendekeza Wananchi kuwa na subira wakati Tume ya Uchunguzi inaendelea kutekeleza hadidu zao za rejea, kisha Serikali itoe taarifa kamili ndani ya muda muafaka kwa uwazi kuhusu Vifo na Mali zilizoharibiwa.
Baada ya kupata taarifa kamili, Serikali yaweza kuandaa pole (ubani) kwa waliofiwa na kutoa misaada wa kiafya na kisaikolojia kwa wahusika wote.
Hatua stahiki zichukuliwe kwa wale watakaobainika kuvuja sheria kupitia vyombo vya kutoa haki.
“Kuhusu Mabadiliko ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania
Kama alivyoahidi Rais Bungeni, uanzishwe tena, mchakato jumuishi, huru na wazi wa mabadiliko ya Katiba, ukihusisha vyama vyote na makundi mbalimbali ya Wananchi
Mchakato uwe na ratiba itakayohitimishwa kwa kura ya Maoni ya Wananchi (Referendum)
Kuna pendekezo la kutofautisha na kutenganisha Mamlaka na shughuli za Serikali dhidi ya Vyama vya Siasa
Wananchi wote tushiriki kikamilifu maana Katiba ndio Sheria Mama na Dira ya namna tunavyotaka kuishi na kujiongoza.
“Kuhusu Uzalendo, Haki na Uwajibikaji
Kila Mtanzania atangulize maslahi ya Taifa juu ya ubinafsi, uchama au makundi yoyote Viongozi wawajibike kwa matendo yao, kuwe na uwazi wa rasilimali na mifumo madhubuti ya usimamizi na udhibiti inayofanya kazi ipaswavyo.
“Hakuna aliye juu ya Sheria, hivyo sote tusimamie utii wa sheria. Tutetee Haki pasipo kuvunja Sheria. Tusimamie Usalama pasipo kujunja sheria! Tulinde Amani bila kuuza Haki.
“Pia Serikali iendelee kusimamia haki na usawa wa raia, ikiwemo kuendelea kuwaachia kupitia taratibu za kisheria wafungwa/mahabusu waliokamatwa kwa sababu za kisiasa.
Sote tupende bidhaa za Nchi yetu na tupende Wataalam wetu katika kutoa huduma kwa umma ikiwa ni pmoja na kutatua kero au migogoro yetu.
“Tusiendekeze majaribio ya utatuzi wa matatizo yetu kwa kutumia Watu wa nje au nchi za nje. Hapa tunarejea wosia wa baba wa Taifa Mwalimu J.K.Nyerere kujongelea utumwa au kutawaliwa kwa kutopenda vyetu.
“Kila Mtazania awe tayari kuwa wazi pasipo hofu ya hofu batiri (phobia- phobia) kuchangia maendeleo na ustawi wa Watanzania ikiwa ni kwa mawazo, ushauri, mali, ujuzi, uzoefu  nk.
Serikali na Taasisi mbalimbali ziendelee kufanya Tafiti za kijamii, kisisasa na kiuchumi ili kueleza matokeo ya tafiti hizo na mapendekezo ya hatua stahiki sanjari na kuibua nyufa zozote zinazojitokeza katika Taifa letu.
“Ujenzi wa Amani, Utatuzi wa Migogoro na Maridhiano
Tunatambua kuwa katika nchi yetu, tunakabiliwa na tatizo la ukosefu wa ajira na kipato kidogo hususani kwa Vijana jambo ambalo ni kero. Sisi Wazee kama Wazazi wa Vijana hao, tunao wajibu wa kuwalea Vijana wetu katika njia zipaswazo na kuishauri Serikali namna bora ya kukabiliana na tatizo hili la kidunia ipaswavyo. Wakati tunashughulikia kero hii na nyingine zozote, tunashauri kuwa na busara katika uwasilishwaji wa kero na kamwe tusikubali kushawishika kutengeneza mazingira ya nchi kutotawalika maana uzoefu umeonesha kuwa madhara yake ni mabaya zaidi na huwa ya kujirudia.
“Chaguo la matumizi ya lugha chafu na matusi huzaa chuki na adhabu badala ya kutatua tatizo lililopo. Sisi wazee tunaamini Watanzania hatujapoteza uwezo wa kutambua changamoto zetu, wala hatujapoteza uwezo wa kuzungumza kwa uhuru, utulivu, kuaminiana  na umoja kutatua kero zinazotukabili.  Hivyo, tunasisitiza kusikiliza malalamiko; kufanya mazungumzo, kutatua migogoro na taratibu za usuluhishi wa kweli kuliko maandamano ya vurugu au yasiyokoma.
Aidha Tunapendekeza kuwa, Tume ya Maridhiano itakapoundwa, iwe na uwakilishi wenye mawanda mapana ya Wajumbe wenye Hekima, Uadilifu na Uzalendo usioshaka ikiongozwa na Raia anayestahiki asiyehusika kuongoza upande wowote wa kisiasa. Aidha Maelezo ya kutosha yawepo wazi kueleza aina ya Maridhiano na Wahusika.
Kila mtu ajiepushe na akemee matamko na vitendo vya kibaguzi au vinavyo hamasisha ubaguzi wowote, uwe wa kidini, kisiasa, ukabila, rika, hali ya uchumi,  tujikite katika kutatua tatizo la ukosefu wa ajira hususan kwa vijana kwa kuboresha será ya ajira, kuongeza sekta za kuongeza ajira, mabadiliko ya mitaala kuendana na soko la ajira, kupanua sekta binafsi zinazotoa ajira na kuwapa vijana stadi anuawai.
Kuunda na kulisimamia Baraza la Vijana la Taifa linalounganisha Vijana wote bila kujali itikadi zao za kisiasa ili kuchochea maendeleo na uzalendo,”amemaliza.
Mkutano huo umeudhuriwa na Wazee kutoka Mikoa ya Tanga, Arusha, Mara, Bukoba, Zanzibar na Dar-es-Salaam.
Leave A Reply