
Tanzania yazidi kupanua miundombinu ya kidijitali, Samia azindua minara 758 ya mawasiliano, atoa tuzo kwa kampuni za simu
Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuimarisha miundombinu ya kidijitali baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kuzindua jumla ya minara 758 ya mawasiliano, katika mpango mkubwa unaolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano na kuharakisha mageuzi ya uchumi wa kidijitali nchini.
Serikali pia imetoa tuzo kwa kampuni za mawasiliano zikiwemo Airtel Tanzania pamoja na Vodacom Tanzania, Yas, TTCL na Halotel kwa mchango wao katika kupanua huduma za kidijitali na kuimarisha mtandao wa mawasiliano nchini, katika hafla iliyofanyika jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alipokea tuzo hiyo kwa niaba ya kampuni yake, akiwakilisha pia wadau wengine wa sekta ya mawasiliano waliotambuliwa kwa mchango wao katika sekta hiyo.
Rais Samia alisema mradi huo umefanikisha kuongeza na kuboresha huduma za mawasiliano kwa takriban wananchi milioni 8.5 katika vijiji 1,400, hatua inayoonesha mafanikio makubwa katika upanuzi wa huduma za kidijitali nchini.
“Leo hii mawasiliano si anasa, bali ni daraja la fursa,” alisema Rais Samia, akisisitiza kuwa serikali itaendelea kuwekeza katika TEHAMA chini ya Dira ya 2050 na Ilani ya CCM ya 2025.
Aidha, alieleza kuwa serikali itaendelea kupanua huduma za intaneti vijijini, kuwekeza katika ubunifu wa vijana, kuanzisha kampuni changa za kidijitali (startups), pamoja na kujenga Kituo cha Umahiri wa Teknolojia ya Kidijitali jijini Dodoma.
Kati ya minara 758 iliyozinduliwa, Airtel Tanzania imejenga minara 169 kupitia mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na binafsi.
Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) ulitoa takriban TZS bilioni 126 kusaidia ujenzi wa miundombinu katika maeneo yasiyo na faida kibiashara.
Mkurugenzi Mtendaji huyo alisema mradi huo unaonesha nguvu ya ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi katika kupunguza pengo la kidijitali nchini.
“Minara hii si miundombinu tu, bali ni nyenzo za fursa zinazowaunganisha wakulima, wanafunzi, wafanyabiashara na jamii kwenye uchumi wa kidijitali,” alisema Kamoto.
Aliongeza kuwa Airtel Tanzania sasa ina zaidi ya vituo 3,700 vya mtandao nchini vyenye huduma za 4G, huku upanuzi wa 5G ukiendelea katika baadhi ya mikoa. Pia kampuni hiyo imejenga zaidi ya kilomita 3,700 za mkongo wa nyaya za fiber optic.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, zaidi ya Watanzania milioni 23 wanatumia huduma za Airtel, ikiwa ni ishara ya ongezeko kubwa la upatikanaji wa mawasiliano nchini.
Kati ya mwaka 2021 hadi 2025, Airtel Tanzania imewekeza takriban dola za Marekani milioni 316 (sawa na TZS bilioni 806) katika miundombinu, imelipa takriban TZS trilioni 1.69 kama kodi na tozo mbalimbali, na kurejesha takriban TZS bilioni 289 kama gawio kwa serikali.
Rais Samia pia alisema hatua ya serikali kuchukua usimamizi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano inalenga kuimarisha uratibu na usimamizi wa miundombinu ya kimkakati ya kidijitali nchini.
Aliielekeza Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kuhakikisha huduma za broadband zinawafikia wananchi wa vijijini na vitongojini, huku akisisitiza umuhimu wa kulinda miundombinu ya mawasiliano na kuzingatia maadili ya kitaifa.
Tuzo zilizotolewa kwa kampuni za mawasiliano zinaonesha umuhimu unaokua wa ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi katika kuimarisha uchumi wa kidijitali, kuongeza ujumuishaji wa kifedha, na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha ICT katika ukanda wa Afrika Mashariki.