
Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu amesema Israel ipo karibu kukamilisha moja ya malengo makubwa ya vita vya Gaza kwa kuwaondoa wote waliohusika kupanga shambulio la Oktoba 7, 2023.
Kauli hiyo imekuja baada ya jeshi la Israel kutangaza kumuua Ezzedine Al-Haddad, kamanda wa kikosi cha kijeshi cha Hamas, kupitia shambulio la anga lililofanyika Gaza siku ya Ijumaa.
Akizungumza katika kikao cha kawaida cha Baraza la Mawaziri Jumapili, Netanyahu alisema alikuwa ameahidi kuwa kila aliyepanga mauaji na utekaji wa mateka katika shambulio hilo angeondolewa mmoja baada ya mwingine.
“Niliahidi kuwa kila aliyepanga mauaji yale na utekaji wa mateka ataondolewa hadi wa mwisho, na sasa tuko karibu sana kukamilisha jukumu hilo,” alisema Netanyahu huku akimtaja Haddad kama “gaidi hatari.”
Shambulio la Oktoba 7 lililosababisha kuanza kwa vita hivyo lilisababisha vifo vya watu 1,221 nchini Israel kwa mujibu wa takwimu rasmi za Israel zilizokusanywa na AFP.
Tangu kuanza kwa vita hivyo, Israel imeendelea kufanya operesheni maalum dhidi ya viongozi wa kisiasa na makamanda wa kijeshi wa Hamas ndani ya Gaza na maeneo mengine ya Mashariki ya Kati.
Katika kipindi cha vita hivyo, Israel imedai kuwaua viongozi kadhaa wa Hamas akiwemo aliyekuwa mkuu wa kisiasa wa kundi hilo Ismail Haniyeh pamoja na Yahya Sinwar ambaye alitajwa kuwa mmoja wa wapangaji wakuu wa shambulio la Oktoba 7.
Aidha, Mohammed Deif, aliyekuwa kamanda wa muda mrefu wa kikosi cha kijeshi cha Hamas, naye aliuawa wakati wa vita hivyo.
Mashambulizi ya Israel pia yamewalenga wanamgambo wa Hamas nchini Lebanon pamoja na makamanda wa Hezbollah wanaoungwa mkono na Iran, akiwemo aliyekuwa kiongozi wa kundi hilo Hassan Nasrallah.
Netanyahu pia alisema majeshi ya Israel kwa sasa yanadhibiti asilimia 60 ya eneo la Gaza, hatua inayotafsiriwa kuwa operesheni za kijeshi zinaendelea kupanuka ndani ya ukanda huo.
Alisisitiza kuwa lengo la Israel ni kuhakikisha Gaza haitakuwa tena tishio kwa usalama wa taifa hilo.
“Tuna Hamas mikononi mwetu. Tunajua hasa kazi yetu ni nini, na kazi yetu ni kuhakikisha Gaza haitakuwa tena tishio kwa Israel,” alisema Netanyahu.
Kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Gaza inayosimamiwa na Hamas, zaidi ya watu 72,763 wameuawa tangu kuanza kwa mashambulizi ya Israel, wengi wao wakiwa raia wa kawaida.
Licha ya makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyoanza Oktoba 10 kwa usimamizi wa Marekani, vurugu bado zinaendelea Gaza huku pande zote mbili zikilaumiana kwa kukiuka makubaliano hayo.
Taarifa zinaonyesha kuwa zaidi ya Wapalestina 871 wameuawa tangu kusitishwa kwa mapigano kuanze, huku jeshi la Israel likisema askari wake watano wamepoteza maisha katika kipindi hicho.