
Watu watatu wamefariki dunia kutokana na kukosa hewa wakati wa sherehe za ushindi wa timu ya taifa ya Mexico katika michuano ya Kombe la Dunia zilizofanyika mjini Mexico City.
Kwa mujibu wa mamlaka za afya za jiji hilo, waliofariki ni msichana mwenye umri wa miaka 19, mwanamke wa miaka 48 na mwanaume wa miaka 44. Wote walipoteza maisha baada ya umati mkubwa wa mashabiki kujitokeza kusherehekea ushindi wa Mexico wa mabao 2-0 dhidi ya Ecuador katika hatua ya mtoano ya michuano hiyo.
Serikali ya Mexico City imesema kuwa zaidi ya watu milioni moja walimiminika mitaani, hasa katika eneo la Angel of Independence katikati mwa jiji, kusherehekea ushindi huo ambao ni wa kwanza kwa Mexico katika hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia tangu mwaka 1986.
Meya wa jiji hilo, Clara Brugada, ametuma salamu za rambirambi kwa familia za waliofariki na kuahidi kuwa serikali ya jiji itatoa msaada kwa waathirika.

Kwa mujibu wa mamlaka ya afya, wahudumu wa dharura waliwahudumia watu watatu waliokuwa wamepoteza fahamu katika maeneo tofauti kandokando ya barabara ya Paseo de la Reforma kabla ya kuwapeleka hospitalini kwa matibabu maalumu.
“Mara baada ya kutoa huduma ya kwanza na kufanya mbinu za kufufua moyo na mapafu (CPR), wagonjwa hao walihamishiwa hospitalini kwa matibabu maalumu,” ilisema taarifa ya mamlaka ya afya.
Hata hivyo, watu hao watatu walithibitishwa kufariki dunia kutokana na kukosa hewa, huku miili yao ikitambuliwa baadaye na familia zao.
Baada ya kutangazwa kwa vifo hivyo, Meya Clara Brugada aliwataka mashabiki kusherehekea kwa uwajibikaji, tahadhari na kuwajali wengine kila wakati ili kuepusha matukio kama hayo siku zijazo.