×

Shakira Kurejea Misri Baada ya Miaka 19, Kutumbuiza Katika Piramidi za Giza

MWANAMUZIKI nyota wa Colombia, Shakira, anatarajiwa kurejea nchini Misri kwa mara ya kwanza baada ya karibu miaka 20, ambapo atafanya tamasha kubwa katika Piramidi za Giza mnamo Novemba 28, 2026.

Tamasha hilo litafanyika katika eneo la kihistoria la UNESCO World Heritage Site, likiratibiwa na kampuni ya Venture Lifestyle. Hii itakuwa ni mara yake ya kwanza kutumbuiza nchini Misri tangu alipoifanya hivyo mwaka 2007 katika eneo hilo hilo maarufu duniani.

Kurejea kwa Shakira kunakuja wakati akiendelea na kampeni ya albamu yake mpya “Las Mujeres Ya No Lloran”, ambayo imeambatana na maonyesho mbalimbali katika nchi tofauti duniani.

Katika zaidi ya miaka 30 ya muziki, Shakira amejiweka miongoni mwa wasanii wa Kilatini waliofanikiwa zaidi duniani. Ameuza zaidi ya nakala milioni 95 za albamu zake, ameshinda tuzo nyingi za Grammy na Latin Grammy, na kuendelea kuvutia mashabiki kupitia muziki wake unaovuka mipaka ya lugha na tamaduni.

Hivi karibuni, Shakira pia aliachia wimbo “Dai Dai”, ambao umejumuishwa kwenye orodha rasmi ya nyimbo za Kombe la Dunia la FIFA 2026.

Akizungumza kuhusu tamasha hilo, Shakira alisema ana furaha kubwa kurejea nchini Misri.

“Nina furaha sana kutumbuiza nchini Misri, katika Piramidi za Giza. Ninawapenda nyote,” alisema nyota huyo wa muziki.

Tamasha hilo linatarajiwa kuvutia maelfu ya mashabiki kutoka Misri na mataifa mbalimbali, huku likiwa moja ya matukio makubwa ya muziki yatakayofanyika Mashariki ya Kati mwaka huu.

Leave a Comment