
Nyota wa Hispania na Barcelona, Lamine Yamal, amekuwa aking’ara duniani akiwa mmoja wa wachezaji bora wa kizazi chake, huku wazazi wake, Mounir Nasraoui na Sheila Ebana, wakiwa nguzo muhimu katika safari yake ya mafanikio.
Yamal alizaliwa Julai 13, 2007 karibu na jiji la Barcelona, Hispania. Baba yake, Mounir Nasraoui, anatokea Morocco, huku mama yake, Sheila Ebana, akiwa na asili ya Equatorial Guinea. Kutokana na asili hiyo, Yamal alikuwa na sifa za kuichezea Hispania, Morocco au Equatorial Guinea, lakini alichagua kuiwakilisha Hispania tangu akiwa katika timu za vijana.
Wazazi wake walitengana alipokuwa na umri wa takribani miaka mitatu. Baada ya hapo, Yamal aliishi zaidi na mama yake mjini Granollers, ambapo Sheila Ebana alifanya kazi katika mgahawa wa chakula cha haraka ili kumlea na kumhudumia mwanawe.

Katika mahojiano ya mwaka 2025, Yamal alisema mama yake awali alitamani amuone akisomea shahada chuoni, lakini yeye alikuwa na ndoto ya kuwa mwanasoka.
“Niliwaambia wazazi wangu, msiponitegemea kwa kazi hakuna shida, lakini nikiwa mwanasoka msihofu, nitakuwa mwanasoka,” alisema Yamal.
Sheila Ebana pia alikuwa na mchango mkubwa katika safari yake ya soka. Kupitia watu aliokutana nao kazini, Yamal alipata nafasi ya kujiunga na akademi ya vijana ya CF La Torreta, ambayo ilimsaidia kuanza safari yake ya kisoka hata pale familia ilipokuwa na changamoto za kifedha.
Kwa sasa, wote wawili wameanzisha familia nyingine. Baba yake Mounir alitangaza uchumba wake na mpenzi wake Kristina mwaka 2025, huku Sheila Ebana akiwa ameolewa tena na kupata mtoto mwingine wa kiume aitwaye Keyne, ambaye mara nyingi huonekana akimshangilia kaka yake uwanjani.

Licha ya kutokuwa pamoja tena, Mounir na Sheila wameendelea kuwa mashabiki wakubwa wa mtoto wao na huonekana mara kwa mara wakihudhuria mechi zake pamoja na hafla muhimu za soka.
Baada ya ushindi wa Hispania katika Euro 2024 na Kombe la Dunia 2026, wazazi hao walikuwa miongoni mwa waliompongeza Yamal, ambaye naye ameendelea kuonyesha upendo mkubwa kwa familia yake.
Akizungumza kuhusu mama yake, Yamal alisema:
“Kwangu, yeye ni malkia wangu na ndiye ninayempenda zaidi.”
Aidha, ili kuheshimu asili ya wazazi wake, Yamal huvaa viatu vyenye bendera za Morocco na Equatorial Guinea, licha ya kuichezea timu ya taifa ya Hispania.
