×

Trump na Netanyahu Waungana Kuishinikiza Saudi Arabia

Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, amesema iwapo Saudi Arabia itajiunga na Makubaliano ya Abraham (Abraham Accords), hatua hiyo itakuwa “hatua ya kihistoria” katika kuimarisha amani katika eneo la Mashariki ya Kati.

Kauli ya Netanyahu imekuja saa chache baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kusema kuwa mkataba wa ushirikiano wa nyuklia kwa matumizi ya kiraia kati ya Marekani na Saudi Arabia utaidhinishwa tu ikiwa Riyadh itakubali kujiunga na Makubaliano ya Abraham.

Hadi sasa, Saudi Arabia haijatoa tamko rasmi kujibu kauli za Trump.

Hata hivyo, Riyadh imekuwa ikisisitiza mara kwa mara kuwa haitaitambua rasmi Israel hadi pale kutakapokuwepo njia ya wazi na yenye kuaminika ya kuanzishwa kwa taifa huru la Palestina.

Makubaliano ya Abraham, yaliyoanzishwa mwaka 2020 kwa upatanishi wa Marekani, yamewezesha baadhi ya mataifa ya Kiarabu kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia na Israel, lakini Saudi Arabia bado haijajiunga na makubaliano hayo.

Leave a Comment