
Baraza la Nchi Wanachama wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) limepiga kura ya kumuondoa madarakani Mwendesha Mashtaka Mkuu wa mahakama hiyo, Karim Khan, kufuatia tuhuma za utovu wa nidhamu wa kingono zinazomkabili.
Hata hivyo, upande wa wanasheria wa Khan umepinga uamuzi huo, ukidai kuwa hatua hiyo imechochewa zaidi na sababu za kisiasa kuliko ushahidi wa kisheria. Wanasheria hao wamesema kuondolewa kwake kumetokea wakati ICC ikiwa chini ya shinikizo kubwa kutoka Marekani na Israel, hasa baada ya Khan kuomba hati za kukamatwa kwa Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, na aliyekuwa Waziri wa Ulinzi, Yoav Gallant, mwaka 2024.
Kiongozi wa timu ya wanasheria wa Khan, Tayab Ali, amesema uchunguzi uliofanywa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Huduma za Usimamizi wa Ndani (OIOS) haukubaini ushahidi wa kuthibitisha kuwa Khan alifanya utovu wa nidhamu au kukiuka wajibu wake.

Ali amesema uamuzi huo haukuzingatia hitimisho la majaji huru waliolichunguza suala hilo, na kuonya kuwa uhuru wa ICC unapaswa kulindwa dhidi ya maamuzi yanayoweza kuathiriwa na maslahi ya kisiasa.
Khan, raia wa Uingereza mwenye umri wa miaka 56, alikuwa ameondoka kwa muda katika nafasi yake mwezi Juni baada ya jopo la usimamizi kueleza kuwa kulikuwa na “utovu mkubwa wa nidhamu” uliokuwa ukichunguzwa.
ICC imetangaza kuwa shughuli za Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu zitaongozwa kwa muda na manaibu wake wawili, Nazhat Shameem Khan na Mame Mandiaye Niang, wakati mchakato wa kumpata mrithi mpya ukiendelea.
Mwanamke aliyewasilisha tuhuma hizo, aliyetambulishwa kwa jina la Sarah, aliiambia CNN kuwa Khan alionyesha tabia ya kumgusa kimapenzi bila ridhaa yake. Hata hivyo, Khan amekanusha madai hayo yote, huku mawakili wake wakisisitiza kuwa mchakato wa kumuondoa haukuwa wa haki na haukuwa na ushahidi wa kutosha.
Kuondolewa kwa Khan kumeanzisha rasmi mchakato wa kumtafuta Mwendesha Mashtaka Mkuu mpya wa ICC, ingawa uchaguzi wa mrithi wake unatarajiwa kufanyika baadaye.