
Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky amesema amekuwa na mazungumzo yenye mafanikio na Rais wa Marekani, Donald Trump, ambapo Marekani imekubali kutoa leseni zitakazoruhusu Ukraine kuzalisha makombora ya kujihami ya Patriot kupitia ushirikiano na kampuni za ulinzi za Marekani.
Akizungumza baada ya mkutano huo uliofanyika Ikulu ya White House mjini Washington, Zelensky alisema pia alikutana na wawakilishi wa kampuni kubwa za kijeshi za Marekani kwa lengo la kuanzisha uzalishaji wa pamoja wa makombora hayo.
Baada ya mazungumzo hayo, Trump aliandika kwenye mitandao ya kijamii kuwa mkutano huo ulikuwa mzuri na kwamba mambo mengi muhimu yalijadiliwa.
Ziara ya Zelensky imekuja wakati Ukraine na Urusi zikiendelea kushambuliana kwa mashambulizi ya masafa marefu, huku juhudi za kidiplomasia zinazoongozwa na Marekani za kumaliza vita hivyo zikiwa hazijazaa matunda.

Kipaumbele kikubwa cha Ukraine ni kupata makombora zaidi ya Patriot ili kukabiliana na mashambulizi ya makombora ya balestiki kutoka Urusi, ambayo yameongezeka katika miezi ya hivi karibuni. Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, mwezi uliopita ulikuwa mbaya zaidi kwa raia wa Ukraine tangu Aprili 2022 kutokana na ongezeko la mashambulizi hayo.
Tangu Trump arejee madarakani, Marekani imesitisha kutoa silaha moja kwa moja kwa Ukraine, lakini imeendelea kuruhusu mataifa ya Ulaya kununua silaha kwa niaba ya Kyiv. Aidha, Washington imeendelea kutoa msaada wa kiintelijensia pamoja na huduma ya mawasiliano ya satelaiti ya Starlink inayotumiwa na jeshi la Ukraine.
Zelensky pia alihudhuria hafla ya kumbukumbu ya Seneta wa Republican, Lindsey Graham, aliyefariki dunia mwezi huu akiwa na umri wa miaka 71. Graham alikuwa mmoja wa wanasiasa waliounga mkono kwa nguvu msaada wa Marekani kwa Ukraine.
Baadaye, Zelensky alizungumza na maseneta wa Marekani kuhusu muswada wa vikwazo vipya dhidi ya Urusi, hatua ambayo alisema ni sehemu ya kuendeleza mpango wa Graham wa kuongeza shinikizo kwa Moscow.
Katika mahojiano na Fox News, Zelensky alisema Rais wa Urusi, Vladimir Putin, amepoteza mwelekeo wa vita kutokana na hasara kubwa za wanajeshi wake.
“Kwa sasa Putin anapoteza takribani wanajeshi 30,000 kila mwezi. Ni hasara kubwa, lakini bado hataki kusitisha vita. Hivyo, mpango wa vita hauko tena mikononi mwa Putin,” alisema Zelensky.
Saa chache kabla ya kukutana na Trump, Ukraine ilifanya mashambulizi makubwa ya mamia ya ndege zisizo na rubani (drones) dhidi ya maeneo mbalimbali nchini Urusi. Wakati huo huo, Urusi iliishambulia Ukraine kwa zaidi ya drones 100 usiku mmoja na kuendelea kulenga bandari ya Odesa pamoja na meli zinazobeba mazao ya kilimo ya Ukraine.