×

Rais Samia Atoa Wito kwa Watanzania Kulinda Amani “Ndiyo Kila Kitu”

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wananchi katika Kilele cha Tamasha la Kizimkazi (Kizimkazi Festival) lililofanyika, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar tarehe 14 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka Watanzania kulinda amani, usalama na utulivu wa nchi, akisema misingi hiyo ni muhimu katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo, Ijumaa, Agosti 14, 2026, wakati akihitimisha Tamasha la Kizimkazi Festival visiwani Zanzibar.

Amesema maendeleo yanayoonekana katika maeneo mbalimbali, ikiwemo uwekezaji, utalii, biashara, ajira na huduma za jamii, yanategemea uwepo wa mazingira yenye amani na utulivu.

Kwa mujibu wa Rais Samia, Watanzania hawapaswi kuichukulia amani waliyonayo kama jambo la kawaida, bali wanapaswa kuilinda kwa nguvu zote ili kuhakikisha nchi inaendelea kusonga mbele.

Amesema mipango ya serikali ya kuvutia uwekezaji, kukuza utalii, kuongeza biashara na kutengeneza fursa za ajira haiwezi kufanikiwa iwapo nchi itaingia katika machafuko na uvunjifu wa amani.

“Uwekezaji, maendeleo tunayoyaona hapa; uwekezaji, utalii, biashara, ajira na huduma za jamii hayawezi kustawi katika mazingira ya vurugu na uvunjifu wa amani. Niwaombe Watanzania wenzangu, hususan vijana, msikubali kuharibu amani ya nchi yenu. Amani ndiyo kila kitu katika maisha yetu,” amesema Dkt. Samia.

Rais Samia amesisitiza kuwa amani ni msingi wa maendeleo na ustawi wa wananchi, hivyo kila Mtanzania ana wajibu wa kuhakikisha utulivu wa nchi unaendelea kulindwa.

Amesema bila amani, shughuli za kiuchumi na kijamii zinaweza kuvurugika, jambo ambalo linaweza kuathiri uwekezaji na fursa mbalimbali zinazotegemewa na wananchi.

Kauli hiyo imekuja wakati serikali ikiendelea kusisitiza umuhimu wa utulivu na mshikamano wa kitaifa katika kuhakikisha Tanzania inaendelea kuvutia uwekezaji na kukuza uchumi.

Rais Samia akiwa kwenye picha ya pamoja na Msanii kutoka Uganda Jose Chameleone katika kilele cha Tamasha la Kizimkazi (Kizimkazi Festival) lililofanyika, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar tarehe 14 Agosti, 2026.

Leave a Comment