×

Vodacom Tanzania Yajenga na Kukarabati Madarasa, Kunufaisha Wanafunzi 4,838

DAR ES SALAAM, Tanzania — 14 Agosti 2026: Vodacom Tanzania kupitia Vodacom Tanzania Foundation imeendelea kuchangia kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto nchini baada ya kujenga na kukarabati madarasa katika shule tatu za msingi za umma mkoani Pwani, Ruvuma na Morogoro.

Mpango huo unaolenga kukidhi mahitaji yaliyobainika katika jamii, umejikita zaidi katika kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto, wakiwemo wenye mahitaji maalum.

Kupitia mpango huo, jumla ya madarasa sita yameboreshwa katika Shule za Msingi Vikindu wilayani Mkuranga, Mahilo mkoani Ruvuma na Ihowanja mkoani Morogoro, ambapo kila shule imepatiwa madarasa mawili.

Kati ya madarasa hayo, mawili yamekarabatiwa huku manne yakijengwa upya. Maboresho hayo yanatarajiwa kuwasaidia wanafunzi 4,838, wakiwemo 117 wenye mahitaji maalum, pamoja na walimu 52.

Mbali na madarasa, shule hizo pia zimepatiwa jumla ya madawati 90.

Hafla ya kwanza ya makabidhiano ilifanyika katika Shule ya Msingi Vikindu, Wilaya ya Mkuranga, ambapo Vodacom Tanzania ilikabidhi madarasa pamoja na madawati yaliyotolewa kupitia mpango huo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Meneja Mauzo Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania, George Nyanda, alisema uboreshaji wa miundombinu hiyo unalenga kuweka mazingira bora zaidi kwa wanafunzi na walimu.

“Katika Shule ya Msingi Vikindu, madarasa haya mawili yanalenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto na kufundishia kwa walimu,” alisema Nyanda.

Alisema kuitikia mahitaji ya jamii kunahitaji kutambua changamoto zinazoweza kuleta tofauti katika maisha ya watoto, hususan wale wenye mahitaji maalum.

Kwa mujibu wa Nyanda, msaada huo utasaidia kuweka mazingira ambayo yatawawezesha wanafunzi kujifunza kwa utulivu na kujisikia kuwa sehemu ya jamii ya shule.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kanda ya Kati wa Vodacom Tanzania, Chiha Nchimbi, alisema madarasa mawili mapya yanayojengwa katika Shule ya Msingi Ihowanja yataongeza nafasi za kujifunzia kwa wanafunzi wa eneo hilo.

“Haya ni maeneo ambayo yatatumika kila siku kwa ajili ya masomo, kukuza ujuzi na kuwawezesha watoto kuendelea kujifunza na kukua,” alisema Nchimbi.

Naye Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wa Vodacom Tanzania, Abednego Mhagama, alisema madarasa mawili mapya katika Shule ya Msingi Mahilo yatawapatia wanafunzi na walimu mazingira bora zaidi ya kujifunzia na kufundishia.

Alisema darasa si jengo pekee, bali ni sehemu ambayo watoto hutumia muda wao mwingi kujifunza na kujiandaa kwa maisha ya baadaye.

Mpango huo utaendelea katika Shule ya Msingi Mahilo mkoani Ruvuma, ambako hafla ya makabidhiano imepangwa kufanyika 20 Agosti 2026, na baadaye katika Shule ya Msingi Ihowanja mkoani Morogoro, 27 Agosti 2026.

Vodacom Tanzania Foundation imesema maboresho hayo ni sehemu ya mchango wake unaoendelea katika kusaidia sekta ya elimu na kuboresha mazingira ya kujifunzia katika jamii mbalimbali nchini.

Foundation hiyo imeeleza kuwa itaendelea kuelekeza juhudi zake katika maeneo yenye mahitaji yaliyobainika, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mipango yake ya kijamii inayolenga kuchangia maendeleo ya jamii na kuongeza fursa kwa watoto kupata mazingira bora ya elimu.

Leave a Comment