×

Serikali Yamjibu Lissu: Sheria Haipo kwa Ajili ya Kumfurahisha Mtu

Dar es Salaam — Mvutano wa hoja umeendelea katika kesi inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu, huku upande wa mashtaka wa Serikali ukisisitiza kuwa mahakama haiwezi kufanya maamuzi kwa misingi ya huruma au shinikizo kutoka kwa upande wowote.

Upande wa Serikali umesema sheria haipo kwa ajili ya kumfurahisha mtu yeyote wala kufuata maombi ya upande fulani, bali mahakama ina wajibu wa kusimamia na kutafsiri sheria.

Mwendesha mashtaka amesema kitendo cha kuielekeza mahakama kwenye hoja za huruma si msingi wa kufanya uamuzi, akidai kuwa Lissu alipaswa kufuata sheria na vifungu vilivyotajwa badala ya kuwaomba majaji wamuone huruma.

Hata hivyo, Lissu amepinga madai hayo na kuwataka mawakili wa Serikali kuonyesha kwenye rekodi sehemu ambayo aliomba kuhurumiwa au kuwatisha majaji.

“Kama nina sehemu yoyote nimesema, ‘Nionee huruma,’ au nimewatisha majaji, basi nionyesheni rekodi,” Lissu amesema, akisisitiza kuwa hakutoa kauli hizo.

Katika hoja nyingine, upande wa Serikali umehoji kauli inayodaiwa kutolewa kuhusu mahakama kushindwa kuwaita mashahidi kwa sababu ya kuihofia Serikali.

Mwendesha mashtaka amesema kauli hiyo inaweza kutafsiriwa kama jaribio la kuishinikiza mahakama na kujenga mazingira ya hofu ambayo yanaweza kuathiri utekelezaji wa majukumu yake.

Serikali pia imesema haikupata hoja yoyote ya msingi katika rekodi za kesi kuhusu mashahidi hao, ikidai kuwa majina yao yalitajwa tu kama sehemu ya mambo mengine yaliyowasilishwa mahakamani.

Kwa msingi huo, upande wa Serikali umesisitiza kuwa Lissu alipaswa kuwasilisha rasmi hoja yake mbele ya mahakama ili majaji waamue kama wana mamlaka ya kuwaita mashahidi hao au la.

Aidha, Serikali imesema suala la iwapo iliogopa au haikuogopa halipaswi kuwa msingi wa uamuzi katika shauri hilo, bali kinachopaswa kuzingatiwa ni sheria, ushahidi na hoja zilizowasilishwa mbele ya mahakama.

Leave a Comment