Dar es Salaam. Tundu Lissu ameiambia Mahakama kuwa John Heche ndiye shahidi wake wa mwisho kutoka miongoni mwa mashahidi raia, akieleza kuwa anatarajia kukamilisha hatua ya re-examination ya shahidi huyo kesho ndani ya muda usiozidi saa moja.
Lissu alitoa kauli hiyo wakati shauri hilo likiendelea Mahakamani, akieleza pia kuwa bado ana mashahidi wengine watatu ambao anahitaji kukutana nao kabla ya kuendelea na hatua inayofuata ya ushahidi.
Kwa mujibu wa Lissu, anahitaji kupata nafasi ya kukutana na mashahidi hao ili kupanga namna ya kuendesha ushahidi uliosalia. Kauli hiyo ilizua vicheko ndani ya ukumbi wa Mahakama.
Awali, Jaji Ndunguru alimweleza Lissu kuwa upande wa utetezi bado una mashahidi watatu na kwamba Mahakama ilitarajia kupokea final submissions siku ya Ijumaa.
Hata hivyo, Lissu aliomba muda wa kukutana na mashahidi hao, akisema hatua hiyo ni muhimu kwa ajili ya kupanga namna ya kuendelea na kesi.
Mashahidi watatu waliobaki ni IGP Camillius Wambura, Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania; CDF Jenerali Jacob John Mkunda, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Wananchi wa Tanzania; na DCI Ramadhan Kingai, Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai.
Baada ya kusikiliza maelezo hayo, Jaji Ndunguru aliahirisha shauri hadi kesho saa tatu kamili asubuhi.
Mahakama pia imebainisha kuwa John Heche bado hajamaliza kutoa ushahidi wake, hivyo hatua ya re-examination ya shahidi huyo inatarajiwa kuendelea kabla ya upande wa utetezi kuwasilisha mashahidi wake wengine.
Hatua hiyo inaendelea huku Mahakama ikiwa imeweka Ijumaa kuwa siku inayotarajiwa kwa upande wa utetezi kuwasilisha hoja zake za mwisho (final submissions), endapo ushahidi utakuwa umekamilika.
